JUMA LA KUMI NA MOJA
Mwaliko wa Kupenda — Mwitikio Wetu
Mwongozo: Kufanya Majitoleo ya Nafsi Kikamilifu

Katika Juma hili tuitikie kwa moyo mwaliko wa mapendo tulioupata. Kupitia katika zoezi la juma lililopita, tumeweza kujua kuwa sifa ya mwitikio wetu inategemea kina cha upendo wetu kwa yule atualikaye.  Pale mpendwa wetu anapotuuliza kuhusu mwitikio wetu kwa mwaliko wake, jibu ni “Ndiyo”.  Hata pale tunapojua kuwa mwitikio huu unaendana na gharama binafsi kubwa sana, bado mwitikio wetu haubadiliki kwa kuwa tunajua upendo daima unatuweka katika ukaribu na umoja wa wapendanao—nasi tunataka daima kuwa na yule tumpendaye.

Kwa mioyo yetu, juma hili tutakuwa tukiitikia mwaliko wa Yesu Kristu.  Tunaweza kwa muda mfupi kufanya marudio ya mwongozo wa zoezi la juma lililopita ili kujikumbusha mwito huu na kuamsha hisia za rohoni tulizopata.  Tuliguswa sana na mwaliko wa kuungana naye katika mradi wa kuwaleta wengi katika kuwakaribisha wengi katika utawala wa Mungu.  Tukiangalia kwa makini, tutaona kuwa mwito huu unatofautiana kidogo kutoka mtu mmoja hadi mwingine kwa kuwa tuna vipaji, historia na malezi tofauti.  Mioyoni, tumezawadiwa neema tofauti baina ya mtu mmoja na mwingine.  Hali ya maisha tuliyopitia; namna mbalimbali za kheri na shari, furaha na huzuni, mahangaiko na starehe; vimetujengea kila mmoja namna tofauti na ya kipekee ya kuhurumia na kuwa na wengine katika magumu yanayowasibu.  Kila mmoja wetu anapata mwaliko kwa namna yake ya pekee, kulingana na umri na uwezo tuliojaliwa hasa wa ushawishi kwa wengine.  Hivi basi tunapenda kusikia mwaliko wa Kristu ukielekezwa kwetu binafsi, kama vile tukialikwa kwa kutajwa majina na yule atupendaye.  Hata hivyo, kwetu sote, kuna usawa katika mwaliko na nafasi tunayopewa ya kuuitia.  Bila shaka mwitikio wetu ni “Ndiyo”.  Hakuna furaha ya kweli maishani ambayo haihusishi kumfuasa Yesu Kristu.  Swali la juma hili ni kina au upevu wa mwitikio wetu—jinsi ambavyo tunaweza kuuitikia kikamilifu mwito wa Kristu.  Hatujui kwa uhakika bayana “Ndiyo” yetu mwaka huu itakuwa namna ipi na itajumuisha yapi.  Kadhalika hatuweze kuwa na habari kamili za “Ndiyo” yetu mwaka ujayo, au miaka kumi kutoka leo.

Hivyo basi, tunaweza kufanya mwitikio ambao bado unaacha mlango wazi—tunajitoa na kukubali kikamilifu lolote lile ambalo ni kumfuasa Kristu. Tunaacha mlango wazi ili kwamba lolote lile limpendezalo Kristu lipate nafasi maishani mwetu. Hata hivyo,  kwa neema ulizopata majuma yaliyopita kutokana na kupendwa na Yesu Kristu, unaweza kuwa umepata shauku halisi ya kupinga lolote ndani yetu ambalo ni la kilimwengu, bure au lililojawa na ubinafsi.

Tunaweza kuwa na shauku ya kujitoa kikamilifu kwa Yesu kwa ubora wa hali ya juu kabisa; na kuwa ishara ya wazi kuwa mwitikio wetu sio wa kuweka viwango, mipaka au vizuizi vya mwisho wa majitoleo yetu.  Ikiwa Bwana wetu atatuchagua, tutaonyesha siyo tu utayari wetu wa kuwa na Kristu katika umaskini wake na kuchukua kwake hali ya kibinadamu, bali pia hamu yetu ya kweli ya kuzisalimisha nafsi zetu tukifuata mfano wake.

Acha picha ya mwalimu na mwanafunzi uliyopewa katika ukurasa huu iwakilishe mwitikio wetu wa kuwa na Yesu katika kuwa na wengine wanaohitaji msaada wetu.  Tumia misaada mingine unayopewa katika juma hili hasa katika kipengele: “Kwa Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...”  Jaribu kuchangia na wenzako neema unazopata juma hili.

Katika juma hili acha maneno na namna zingine za kuelezea mwitikio wako kwa mwito wa Yesu zibubujike bila kipingamizi kutoka moyoni mwako.  Una majuma mengi zaidi mbele yako ya kukua katika shauku ya kupenda zaidi na kuendelea kuchunguza kina cha majitoleo yetu.  Juma hili tujaribu kutafakari mwitikio wetu kwa kadiri tulivyoneemeshwa kujitolea.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili

Kumsaidia mtu kuitikia mwaliko binafsi wa mapendo kwa kiasi fulani ni kama kumsaidia mtu kuchagua zawadi ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya ampendaye, au ya kumbukumbu ya miaka fulani baada ya tukio muhimu kama vile ndoa, upadrisho nk.  Maswali yanayojitokeza yanaweza kuwa haya: uhusiano wake na mtu huyu ni wa karibu kiasi gani?  Kiasi gani cha fedha yupo tayari kutumia?  Angependa zawadi hii ifikishe ujumbe gani?  Na wewe pia katika umbali uliokwenda katika mafungo haya, maswali yanayotegemewa kukujia ni kama haya:

·       Ni kwa undani kiasi gani nimeguswa na na upendo na huruma ya Mungu?

·       Ni kiasi gani ninajawa na moyo wa kutaka kuonyesha shukrani?

·       Ni kwa undani kiasi gani nilisikia mwito na mwaliko wa Yesu?

·       Ni mwitikio gani “unaumbika” moyoni mwangu?

 

Ushauri wa kwanza kwa juma hili ni kuanza na mwitikio ulio rahisi kuliko yote.  Sema ndiyo.  Jaribu kufanya zoezi la kusema “ndiyo” kwa sauti.  Je, una unajisikia vipi unapoisema ndiyo yako kwa namna tofauti tofauti (kama vile: sawa, naam! Enhee!, nipo..., nk) ?  Unaiihisi namna mbalimbali za kiwango cha ukweli wa mwitikio wako?

Zoezi linalofuata laweza kuwa katika hali maalum au inayoendana zaidi na ndiyo yako.  Naweza kusema ndiyo na kuwa na maana kuwa kumfuasa kwangu Yesu katika kutekeleza kazi maalum aliyotumwa na Mungu Baba ni kuwa mwaminifu katika lolote linijialo leo.

Naweza kuhisi kuwa kuna aina maalumu ya uaminifu ambayo imeambatanishwa na mwaliko wa Kristu kwangu; kwa mfano uaminifu katika maagano ya matakatifu ya ndoa.  Hivyo basi itabidi ndiyo yangu iwe mahususi: “Ndiyo, nitakuwa nawe katika uzito wote wa uaminifu wa kumpenda mwenzangu wa ndoa”  au “...katika kuwapenda watoto wangu”.  Kwa wengine, kutokana na umaalumu wa mialiko yao, miitikio yao inaweza kuwa: uaminifu katika kupokea na kukubali changamoto zote za kazini,  ...msamaha kwa ndugu au jirani nk. Wakati mwingine mwitikio waweza kuwa katika hali ya kubadili hali au tabia ambayo inapingana na mwito wetu maalum.

Zaidi, naweza kujikuta nikialikwa kwenda sehemu ambapo niliusikia mwito, lakini sikuuitikia.  Naweza pia kuifanya ndiyo yangu ibaki “mlango  waz”i zaidi, yaani kutokuwa na umaalumu wowote isipokuwa kumfuasa Kristu; “Ndiyo, nataka kuwa nawe katika hali ya kupenda kama wewe, na nitaufungua moyo wangu wazi kabisa kutoa msaada kwa wowote wanaouhitaji, hususan maskini.”  Vilevile naweza kuweka na kuitekeleza dhamiri ya kujihusisha zaidi katika mwaliko wa kulitumikia Kanisa la Kristu.

Kunaweza kuwa hamu au mvuto wa pekee unaojengeke moyoni mwangu wa kuitikia upendo wa Yesu ambao siku baada ya siku unaongezeka katika kujibainisha moyoni mwangu, hadi kufikia hali ambayo moyo wangu unaanza kushabihiana na wa Kristu.  Naweza kujaribu kutumia maneno ya mtu aliye katika mahaba na Kristu, yaliyo na mguso wa pekee ndani kabisa moyoni.  Naweza pia kujaribu kujiweka karibu kabisa na Kristu ili kushirikishwa unyenyekevu wake alipojishusha na kuwa mwanadamu katika hali na wakati wa umaskini wa kila namna, na kuacha nikuguswe na unyenyekevu huu hata kujihisi nashiriki hali yake.  Kama wapendanao watendavyo, naweza kutamani kuuweka moyo wangu ndani ya wake mtakatifu.  Naweza kufanya mazoezi ya kusema kwa sauti, au kwa kuandika katika daftari huku kukua kwa shauku yangu ya kumjua Yesu Kristu na kuingia katika mahangaiko na umasikini na kujisalimisha kunakoujaza Moyo wa Yule Ninayempenda.  Hapa, ndiyo na kiu yangu ya kuwa karibu na Kristu vinaunganika au kufanya makutano.

Katika majuma yafuatayo, tutatafakari yafuatayo:

·       hamu au kiu ya kuukua katika kumjua Yesu,

·       kukua katika upendo wa karibu zaidi na Yesu, na

·       kuwa pamoja katika kumtumikia Yesu.

 

Katika juma hili tuna uhuru wa kuacha ufahamu wa kila mmoja wetu kwenda sehemu zozote ambazo “mpenda mwenye shukrani anaweza kuzichukua kama njia ya kusema ndiyo  kwa mwito wa “mpendwa” wake.

Kama tufanyavyo kila juma, tuache neema tunazosaka zidumu katika ufahamu wetu tangu wakati tuamkapo, tukiwa kazini au katika shughuli zingine za siku, hadi wakati tunapojiandaa kulala.  Naweza kujizoeza kuvuta pumzi taratibu, hadi kunijaza kabisa na kupumu taratibu huku nikipitia jambo moja hadi jingine, wakati nikijianda kwenda kazini.  Pumzi hiyo ya taratibu ila ipenyayo ndani kabisa, yaweza kuwa ndiyo yangu kutoka ndani kabisa moyoni: Kuvuta pumzi, napokea mwaliko na kuitoa pumzi, nasema ndiyo.  Fanya mazoezi ya kufanya mwitikio wako yakujaze au kukuzingira wewe mzima, mipango, dhamira, mategemeo, hisia n.k. za kila siku.  Vilevile, hisi nguvu ambayo inaweza kutokana na kuongezeka kwa hali ya kupenda.

Kwa Ajili ya Safari:
Kuingia Kwenye Ufalme wa Kristu


Katika kadi nyingi za mwaliko kuna kipengele kisemacho: “Majibu kwa Wasiofika...” kikiwa na maana kuwa iwapo una udhuru wa kutokuweza kuitikia mwaliko, basi umwarifu aliyekualika au wakala wake ambaye kawaida anuani yake na namba ya simu vimeambatanishwa.  Tupokeapo mwaliko kama huo, kwanza tunachunguza iwapo tunao muda wa kuhudhuria mwaliko huo na iwapo tuko tayari kwenda tunapoalikwa.  Mara nyingine katika mialiko fulani hakuna chochote cha kujiuliza:  “Nitaweezaje hata kufikiria jinsi ambavyo naweza kuacha kuitikia mwaliko huu!”

Kipengele cha kuomba majibu kama kile cha “Majibu kwa Wasiofika...” kipo katika hali-fiche katika zawadi nyingi na sauti nyingi ambaza Mungu huzitumia kutuita.  Kuna namna mbili ya kuitikia mwaliko unapofikishwa kwetu.  Ya kwanza ni kutoa jibu baada ya kuwaza; kuangalia faida na muda, hasara na gharama; kuchanganua maana na uzito hasa ya mwaliko wenyewe na kiini chake; kuchunguza matokeo yakinifu ya kutokuhudhuria na ya kuhudhuria n.k.  Namna ya pili ya kuitikia mwaliko inatokana na hisia za ndani na uamuzi hufanyika mara, bila kuwaza wala kuwazua.

Mara moja kila mwaka, Kanisa Katoliki husherehekea sikukuu ya Yesu Kristu Mfalme.  Kristu anatujia kama mfalme-mtumishi na vilevile kama mfalme-mwalikaji—huwaalika watu wote katika utumishi kwa wote anaowaalika kwake, yaani “ulimwengu mzima”.  Tunakaribishwa na Mt. Inyasi kutafakari namna nyingi ambazo tayari zimetumika na Kristu katika maisha yetu kutuita kuingia ndani zaidi ya Ufalme wake.  Katika kutuumba, Mungu katujaza zawadi nyingi na talanta za kila namna.  Mwito wa Mfalme katika Mazoezi ya Kiroho unatusihi tumwitikie Mfalme kwa kutumia zawadi tulizopewa katika kuumbwa kwetu na zilizoendelea kuongezeka katika maisha yetu.  Kristu aliwaalika wavuvi wa samaki kuwa wavuvi wa roho:  vilevile anatualika kila mmoja wetu kuuitikia mwito wake kufuatana jinsi alivyo pamoja na vipawa alivyojaliwa.  Anasema “ nakualika wewe kufanya jambo fulani kwa kuwa nimekujalia tayari karama hii na talanta ile ya kutenda jambo hili ninalokuitia.”  Mwito wa Kristu basi unatuthibitishia kuwa ni yeye aliyetupa tulivyonavyo, ni baraka kwa kutuonyesha jinsi alivyotubariki na jinsi ya kuzitumia baraka hizo; na ni zawadi kwa kutuonyesha matumizi ya faida na maana ya juu kabisa ya zawadi alizotujalia Muumba wetu.

Sali ukimsikiliza Kristu akikuita.  Acha maneno yake yaingie sana akilini na moyoni mwako hata uwe kama unayesikiliza wimbo au muziki mzuri sasa wenye maneno kama haya: “Njoo kwangu... Nifuate.  “Nitendalo, na liwe tendo lako... “Nitamkalo, na liwe Neno lako... “Nikilacho, na kiwe chakula chako... Nikinywacho, kikate kiu yako... Nilalapo, na pawe malazi yako... chukua mkono wangu, niangalie machoni na uniambie utanifuata daima... nipe moyo wako, niuweke Moyoni mwangu... kwa kuwa Moyo wangu una nafasi kubwa kwa ajili yako, na Nyumba ya Baba Yangu ina vyumba vingi saaana.

Yesu anatusihi tumfuase, ila kumfuasa huku hakuna maana ya kufuata “njia” tu yake yeye akiwa hayupo.  Kumfuasa Yesu ni kuambatana naye na kushirikiana naye katika yote: atakuwa nasi na kutenda kazi pamoja nasi, atatenda mengi kwa kupitia vipawa na uwezo wetu, na hatatuomba kutenda lolote lile ambalo yeye mwenyewe hayuko tayari kulitenda.  Anatukaribisha katika ushindi wake, ila pia katika hali yake ya kibinadamu kabisa ya kuupata ushindi huo.

Tunaombwa kutafakari kuhusu yale yanayotugharimu katika kumfuasa Kristu.  Baada ya kufanya hivyo, tujaribu kusikiliza kutoka ndani kabisa mioyoni mwetu, sauti ya Mungu ikituita kwa upole kujitolea sisi wenyewe na zawadi zote alizotupa Mungu—vyote viwe zana ya kumfuasa.

Ni kweli tunaweza kuwa na nia na shauku kuu, lakini ukweli wa kibinadamu ni kuwa kwa nguvu zetu wenyewe, hatuwezi kuyatoa maisha yetu kikamilifu kwa Mungu bila kurudi nyuma.  Petro, wa kwanza kati ya wavuvi wakubwa wa watu, aliacha yote ili kumfuata Yesu, na kwa miaka mitatu tunamwona akisitasita na kuonyesha woga.  Katika Injili tunamwona Petro akimsihi Yesu asiende Yerusalemu kwani kulikuwa mahali pa hatari wakati huo, akitoa ahadi ya kutokumkimbia Yesu lakini akimkimbia alipowekwa nguvuni, akimkana mara tatu katika njia ya msalaba, na akiwashauri wenzake kwenda kuvua samaki, baada ya ufufuko wa Kristu nk.  Ni kweli bado alimpenda Yesu, na hatusiti kusema kuwa alipenda kutoa maisha yake yote kuitikia mwito wa Yesu, lakini bado alijikuta na udhaifu wa kibinadamu, udhaifu ambao ni pengo linaloweza kujazwa na Mungu pekee.  Kila mmoja wetu ana wakati ambao anatamani kuyaweka mikononi mwa Kristu maisha yake na yote aliyonayo.  Tusisite, na wala tusione ni kidogo kile tunachomtolea—tujue kuwa yeye atapokea sehemu yoyote ya mioyo yetu, talanta zetu, na maisha yetu ambayo tunaweza na tuko tayari kumtolea.


Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...

Bwana Mpendwa,

Nahisi mwaliko wako ndani kabisa ya roho yangu.  Katika ukimya, natulia nikijawa na shauku kuu ya kuitikia mwito ambao haujajibiwa maishani mwangu, na naona waziwazi kuwa kwenye mwaliko wako unaoutoa kwa kwa moyo mnyenyekevu ndipo pekee penye jibu.

Nakuhisi ukiniita na kunialika—ukijitolea kujaza sehemu tupu ndani yangu inaosababishwa na kuipuuza shauku ya kuitikia mwito wako.  Utupu huu umejificha ndani yangu, mahali ambapo ni wewe tu, Mungu wangu, ndiye unayeweza kupafikia na kustahili kufanya makao yako, mahali pa kuwa nami mpendwa wako.  Inakuwa vipi kwamba mwaliko huu unauelekeza kwa nafsi yangu kiasi hicho, hata ukinitaja mimi kwa jina na kunijia katika hali isiyopingana na yote yangu yaliyo mazuri—elimu yangu, umri wangu, uwezo wangu, ujuzi wangu, mahali ninapoishi...?  Tazama sina jibu jingine kwako ila “ndiyo”.  Nawezaje kuwa na jibu tofauti na hilo, baada ya kushuhudia ukarimu wako, uaminifu wako kwangu na upendo mkubwa ulionionyesha katika maisha yangu?

Sijui ndiyo yangu itanipeleka wapi.  Mwaliko wako hauna shuruti wala vitisho vyovyote, na sina woga wowote.  Unanisihi, kwa kiasi fulani, kubadili mtazamo wa maisha yangu ili kwamba niwe kwa kiasi kikubwa kama ulivyoniumba, na siyo mimi ninayeiga hali za wengine nikionea aibu fulani uumbaji wako.  Mimi ni mwema nilivyo na unanipenda katika hali njema uliyoniumbia.  Kwa kiasi fulani, nakiri kuwa na woga ninapoanza kuwaza wapi hasa haya yote yananiongoza na ni kwa kiasi gani yanaweza kubadili maisha yangu.  Hata hivyo, kwa namna fulani, najua kama nikiitikia mwito wako nitakuwa jinsi ulivyotaka mimi niwe wakati uliponiumba.  Nitakuwa mimi hasa, nafsi yangu ikinionyesha mimi halisi bila ubandia wowote.

Naanza kuelewa, Bwana Wangu, kubwa si matokeo ya ndiyo yangu tu ambayo ni muhimu.  Muhimu zaidi ni ndiyo yangu.  Ni kiu au shauku ya kuwa nawe ndani yangu ili kukidhi hamu ya kutaka kukufuasa, kutuliza njaa ya kukutumikia wewe katika hali yoyote utakayonionyesha.

Nitamani kuwa na shauku ya kweli ya kujisalimisha kwako mimi mzima na yote yaliyo yangu.  Nisadie Bwana Wangu, kutokurudi nyuma katika ndiyo yangu.  Nipe nafasi niung’ang’anie mkono wako, na kusonga mbele nawe bila woga.

Nasema asante kwa yote uliyonijalia.  Nasema ndiyo kwa yote utakayonijalia.

Ndiyo, Bwana wangu.  Niite, mwitikio wangu ni ndiyo Bwana, mimi hapa niko tayari...

Ndiyo, NDIYO! Milele Ndiyo!

Amina.

Maandiko Matakatifu

Isaya 6:1-8

Zaburi 116

Luka 10:1-9; 17-21

Yohana 21:15-19

 

MAFUNGO YA KIROHO KUPITIA MTANDAO