JUMA LA KUMI NA SITA

Maisha Nje ya Hadhara kwa Miaka Thelathini

Mwongozo: Mwana wa Seremala

Mojawapo ya ukweli wa kushangaza sana kumhusu Yesu Kristu ni kuwa tunajua kidogo sana kuhusu maisha yake katika miaka thelathini ya mwanzo wa maisha yake. Tunajua alipoanza kazi yake hadharani, wali walimjua yeye na ndugu zake walishangazwa sana.  Kwa dharau wengine walitoa mashambulio yao dhidi yake wakisemezana: “huyu siye yule mwana wa seremala?”

Juma hili la mafungo linatupa muda wa kumjua Yesu anayekua katika ubinadamu wake (anayeongezeka umri).  Kwa kuwa kuna Maandiko machache sana ya kurejea kuhusu maisha yake kati ya kuzaliwa kwake na kubatizwa kwake, tutatumia ubunifu wetu kujazia sehemu zile ambazo hatuambiwi mengi na maandiko—ila tunajua kweli mbalimbali za historia ya wakati huo, kazi ya baba yake, imani na tamaduni za watu wake, n.k. Zaidi, kama tukiifikiria hali ya utu-uzima ambayo Yesu alifikia, tunaweza pia kutafakari jinsi utoto wake ulivyokuwa, alikuwa mtoto wa namna gani, mambo gani alipambana nayo katika maisha na fikara, ni maamuzi gani hasa alifanya, n.k. Kwa kutumia kile tunachojua kuhusu maendeleo ya watoto hadi kufikia ujana, halafu kufikia utu uzima, tunaweza kufanya ubunifu mzuri kuhusu mambo kadhaa ya kibinadamu ambayo sharti Yesu aliyakabili. Tukisali namna hii tuingie katika zoezi la kumjua kwa undani zaidi, ili kwamba tuweze kumpenda zaidi na kufikia shauku yetu ya ndani kabisa ya kuwa naye katika utume wake aliopewa na Mungu Baba.

Tufungue mioyo yetu ili tuonyeshwe jinsi ilivyokuwa miaka ya utoto wa awali wa Yesu.  Tunaweza katika juma hili kuenenda tukitafakari magumu yote ya kibinadamu yaliousibu utoto wa Yesu? Na tunapofikia miaka yake ya kubalehe na ujana, tunaweza kumpa nafasi atuambie aliipitia vipi na kuwa mtu tunayemjua sasa.  Tunaweza kutafakari mahangaiko na harakati alizokuwa nazo?  Vipi kuhusu maswali aliyojiuliza?  Yapi yalikuwa mazito kwake? Wapi alikuwa na nguvu na wapi alikuwa na madhaifu? Tunaweza kudhani mahusiano yake na watu katika hatua mbalimbali za kukua kwake?

Kama tunaweza kupata mengi kumhusu Yesu katika miaka yake ambayo haonekani hadharani, tunaweza pia kujifunza mengi kuhusu jinsi Mariamu na Yusufu walivyomlea.  Tunaweza kutafakari jinsi maisha katika mji wa Nazareti yalivyokuwa.

Tunajua kuwa Yesu alijiona na kujijua kama aliyeitwa kutangaza wokovu kwa wote utumwani na kutangaza Habari Njema kwa maskini.  Tunajua kuwa alitambua kubarikiwa kwa aliye maskini wa roho.  Tunajua kuwa alijua kuwa utawala wa Mungu ni kama chachu ya kuumulia unga au mbengu ndogo, na kuwa magugu na ngano sharti vikue pamoja.  Tunajua kuwa hakuogopa kula na kunjwa pamoja na wenye dhambi na wale ambao welikwepwa na kutengwa na viongozi wa dini. Tunajua kuwa alijiona kama mtumishi, mwoshaji wa miguu ya watu, na mkate ambao utamegwa na kutolewa [kafara] kwa ajili ya maisha ya ulimwengu.  Ilikuwaje mwana wa seremala ayafikie haya yote?

Hakika mtu anayetupenda atatuonyesha yeye ni nani, atatupa nafasi tumpende zaidi kuliko tunavyoweza kudhani na kutuvutia kumfuasa kwa karibu zaidi, siku baada ya siku, wiki baada ya wiki.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili

Kutafakari maisha ya Yesu yaliyojifichika kunaweza kuwa na changamoto nyingi mwanzoni.  Tunaweza kuogopa kwa sababu ya kutokuwa na simulizi za kutosha za maandiko matakatifu kuhusu sehemu hii ya maisha ya Yesu, hivyo tafakari yetu inaonekana tofauti na tuliyozoea ya Neno la Mungu tunalosoma kutoka katika Biblia.  Ila kwa kutumia uwezo wa udhanifu wetu na uhuru tulionao—na kwa kutumia nguvu tunayopata baada ya kuguswa na Yesu ndani mioyoni mwetu—juma hili linaweza kuwa na uzuri wa kustaajabisha.  Zaidi, kufanya mazoezi haya katika mazingira ya maisha na mishughuliko yetu ya kila siku kunaweza kuwa chanzo cha neema zenye nguvu.  Zana za Kukusaidia katika majuma mawili yaliyopita zilikuwa na ushauri wa msingi kwa ajili ya kusali kwa kutafakari aya za Maandiko Matakatifu, katika kipindi maalum cha sala na pia katika hali ya kawaida ya kuendelea na maisha ya kila siku.

Tunaweza kuanza kwa shughuli ya ndani ya kukusanya habari yakini.  Tunajua nini kuhusu jinsi watoto wachanga wanaendelea kuwa watoto wavulana au wasichana wadogo, na jinsi wavulana watoto wadogo wanavyokua kufikia muda wa kubalehe, kisha kuwa kufikia ujana na mwishowe kukomaa katika utu uzima?  Tunajua kuwa hatua za kukua zinahusisha changamoto na migogoro mingi.  Tunajua kuwa katika haya yote wazazi ni wa muhimu sana. Tunajua pia kuwa marafiki wa rika moja ni muhimu katika kukua.  Zaidi, tunajua kuwa uamuzi wa awali wa mwelekeo wa maisha yetu hutuumbia mazingira ya baadaye ambapo chaguzi na maamuzi mbalimbali hutendeka.  Yesu, hakika alipitia hatua zote hizi katika kukua kwake.  Mwinjili Luka anatuambia, “Mtoto Yesu alipokuwa akikua, alijawa na busara na baraka ya Mungu ilikuwa naye” (Luka 2:40).

Sasa kuyaweka katika umbo yote tunayokusanya kuhusu miaka ya kukua kwa Yesu Kristu, tujaribu kuangalia alikuja kuwa mtu wa namna gani.  Ukweli ni kwamba zoezi hili huwa tunalifanya kila mara.  Tunamwangali mtu, hasa mtu tunayemchukia au yule ambaye tunadhani hajakua mtu mzuri kiasi cha kutupendeza, na tunaanza kufanya dhana au ubunifu wa jinsi utoto wa mtu huyo ulivyokuwa.  Pia tunaweza kukutana na mwanafunzi mwenzetu chuoni ambaye ana kila tabia tunayodhani ni nzuri, na kujiambia kuwa wazazi wake sharti walitenda vema katika kumlea.

Injili inatusaidia kujua Yesu ni nani leo hii.  Ni nani huyu anayenipenda mimi leo, Yesu ninayezungumza naye katika sala na aliye na makovu na matundu katika viganja vyake?  Tunajua hawakwepi wadhambi na wanawake na wengine ambao jamii ya wakati wetu haiwapi nafasi vya kutosha. Tunajua kwamba anayajua maisha ya kila siku: kwa mfano alitumia mifano iliyohusiana na kuoka mikate, ukulima au utunzaji mimea, kualikwa na kwenda harusini, na kuhusu jinsi watu hutupata mali na kuitunza.

Sasa tupo tayari kuziweka katika uhalisi tafakari zetu kwa kuunda matukio. Tunaweza kuanza kwa kuitengeneza picha ya jinsi nyumba ya Mariamu na Yusufu ilivyoweza kuwa.  Inasaidia kupata habari nyingi na kwa kinaganaga iwezekanavyo.  Ina vyumba vingapi? Vyumba vina ukubwa kiasi gani?  Ni nini kinachotendeka katika kila chumba?  Kuna samani gani katika kila chumba?  Ni wapi wanapolala, wanapolia chakula, wanapopikia, wanapokaribishia wageni? Ni wapi ilipo karakana ya useremala ya Yusufu?  Karakana ya Yusufu ikoje?  Kisha tunaweza kuunda picha ya mpangilio wa mji mdogo Nazareti.  Watoto wanacheza wapi?  Kisima cha maji kiko wapi?  Sinagogi wanapoenda siku ya Sabato lipo wapi?  Soko la mji liko wapi? Na ukumbi wa harusi upo wapi? Makaburi yao yako wapi?

Sasa tupo tayari kuyatazama matukio ya kawaida ambayo hakika yalitokea katika maisha ya Yesu.  Jinsi tunavyoyadhani na kutafakari uhalisi wa maisha ya Yesu, tuingie ndani yake hadi kuwa sehemu ya wahusika katika matukio ya maisha yake, tukiyaishi matukio katika maisha yake na kujifunza mengi kumhusu Yesu, na kumsikiliza akituambia lolote analotaka kutufunulia.  Tunawea kujiundia picha ya mgogoro au tatizo lolote maishani, kuchanganyikiwa kunakotokea wakati ambapo inabidi tuchague njia fulani ya maisha ambapo gharama yake ni kuacha au kupoteza chaguo jingine; au pia tunaweza kuchukua jambo lililowahi kutugusa sana moyoni katika maisha yetu.  Uzuri wa namna hii ya tafakari ni kuwa siyo kila kipengele chake kinapaswa kuwa na ukweli kamili wa kihistoria.  Mada tunayoishughulikia inatupa mazingira na mlango wa kuingia katika sehemu ya kukutania na kuzungumza au kuwa na Yesu uso kwa uso.

Kuna matukio mengine zaidi ambayo tunaweza kuyajenga au kuyaendeleza: hapo mwanzo kabisa wa maisha ya mtoto Yesu ambapo Mariamu na Yusufu walikuwa wakijifunza kumtunza Yesu, kumlisha, kumvika mavazi ya kitoto; Matukio ya kumfundisha kuzungumza na kutembea; Matendo iliyobidi wayafanye kumfundisha Yesu, kumsahihisha, kumfunza nidhamu;  Matukio ya mezani walipokula chakula, nyumbani alipocheza na kuigiza watu mbalimbali waliomvutia, muda wa kusali;  Yesu akijifunza kusoma; Wakienda naye kwa mara ya kwanza katika sherehe ya harusi, wakienda naye kwa mara ya kwanza katika mazishi; Yesu anapoanza kwa mara ya kwanza kusaidia katika karakana ya useremala; Yesu anapokuwa kwa mara ya kwanza katika kikundi cha marafiki wavulana wadogo, migogoro midogo midogo inayotokea katika kikundi chao cha urafiki;  Baada ya kubalehe—Yesu anapokutana kwa mara ya kwanza na wasichana na mambo aliyoyakabili katika muda huu wa maisha yake; jinsi familia yake ilivyotatua migogoro ya kawaida kati ya familia yake na ndugu au majirani; Yesu kama msaidizi wa fundi seremala, aliposaidia katika kupeleka kazi kamilifu kwa waliagiza au walionunua, alipojenga nyumba;  jinsi familia ilivyoshughulikia masuala ya kuzeeka, kuumwa na kufariki kwa Yusufu.

Hapo mwanzo ilionekana kuwa hakukuwa na chochote cha kutafakari, kwa sababu ya ukweli kuwa  maisha yake yalikuwa yamefichika.  Sasa tunaona katika muda huu kuna mengi sana ya kujifunza kumhusu Yesu.  Hakuna hata mmoja kati yetu anaweza kupata muda kwa ajili ya yote haya, hususan juma hili, ila ni neema kubwa kupata mlango wa kuingia katika maisha ya Yesu na kumpa nafasi atuambie jambo kujihusu yeye mwenyewe.  Hii inawezekana hata katika harakati nyingi za kazi na maisha yetu kila siku kwa kadiri tunavyoendelea kuvutiwa na Yesu.

Katika juma hili fikara na tafakari zetu zijazwe na yote tutakayopitia kuhusu maisha ya Yesu na nafsi ambayo maisha yake yalimjengea.  Tunapoliishi juma hili la mafungo, tutaona kuwa, kuunganisha kwetu sala na yale tunayotenda au kutendewa, kusema au kuambiwa, n.k. kunaleta mshahibiano na yale tunayowaza kuhusu maisha ya Yesu kwa kuwa Yesu pia aliishi kama katika maisha yetu kila siku, akitenda kazi na kushirikiana na wengine, akizungumza na kusikiliza wengine, akiwaza, akifurahi na kuwa na hisia mbalimbali za kibinadamu.  Hii ni kusema juma hili tutakuwa tumezama hasa katika sala ya tafakari kwa kuwa tutakuwa na Yesu ambaye pia anashughulika nasi kila siku.  Magumu yote ya kawaida tunayokutana nayo katika maisha yataonyesha maisha ya Yesu kuwa ya kibinadamu na halisi kwetu, na wala siyo ya dunia nyingine wala simulizi za kutunga tu.  Hii itatusogeza zaidi na zaidi karibu naye.

Kwa Ajili ya Safari: Kuwa Karibu Zaidi na Yesu

Tunaanza juma hili kwa kusikiliza na kutazama matukio katika maisha ya siku za awali ya Yesu.  Wachungaji kondoo na mamajusi, maskini na matajiri, wamefika kumwona yule ambaye amekuja kutusaidia kujiona na kujitambua binafsi. Neno limesemwa katika Mji wa Daudi, na Neno linatayarishwa ili kusikiwa na wote, Wayahudi na Watu wa Mataifa, karibu na mbali, masikini kwa matajiri.

Yusufu, ambaye alisihiwa na malaika matika ndoto kumchukua Mariamu awe mke wake, sasa katika ndoto anaambiwa amchukue Mariamu na mtoto wao waende kwenye nchi ya mbali.  Hapa tunashauriwa kutilia maanani imani aliyokuwa nayo kumwezesha kuzisadiki ndoto hizo na imani aliyokuwa nayo kuzisichukulia kama ombi au mwaliko na siyo amri au shuruti.  Kusafiri, bila kujua kwa uhakika tunakoelekea na kwa sababu gani hasa kunaelekea kuwa mada na kiini cha yanayotokea hapa mwanzo katika maisha ya familia takatifu.  Wachungaji kondoo wamerudi katika shughuli zao wakimtukuza Mungu; wafalme (mamajusi) wamerudi walikotokea wakitafakari yale waliyoyashuhudia;  Mariamu, Yusufu na mzigo wao wa ajabu wanabaki peke yao na kusafiri kuelekea Misri ambapo wanangojea maelekezo zaidi, ambayo wanaamini watapewa muda utakapofika.

Tunakaribishwa kutembelea hekalu miaka kumi na mbili baadaye, katika muda ambao Yusufu, Mariamu na Yesu katika utatu wao wanasafiri kwenda Yerusalemu.  Kinachotokea ni kuwa wanaanza safari ya kurudi nyumbani bila kuwa na Yesu, na wanashtuka sana na kuogopa kama wazazi wanapogundua hili.  Hapa mtakatifu Inyasi anatusihi tusikilize na kutafakari hisia zao:

Ikawa baada ya siku tatu walimkuta hekaluni akizungumza na walimu wa dini na sheria: “Na walipomwona walishangaa na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. Akawambia, “Kwa nini kunitafuta?  Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwemo katika nyumba ya Baba yangu?  Akashuka pamoja nao Nazareti, naye alikuwa akiwatii, na mamaye aliweka haya yote moyoni (Luka 2:48/49)”

Wanamkuta Yesu, akiwa anaonekana hazijali hisia zao wazazi wake.  Yesu kakamilisha sheria ya kuwatii wazazi wake na sasa anatekeleza sheria mpya ya kumtii Baba yake wa mbinguni.  Ilimbidi atekeleze utume wa Baba yake, kazi ambayo inakuwa ya kudumu maisha yake yote: anaishi akisema na kutenda maneno ya Mungu.

Tunatazama kwa uangalifu kuvurugikiwa kwa hisia katika mioyo ya Mariamu na Yusufu. Mshangao: “Kwa nini!” anaoutoa Yesu unabadilika na kuwa swali zuri sana: “Kwa nini?” Mariamu atajiuliza swali hili mara nyingi katika maisha yake.  Tunategemea kwamba alisali ili kwamba maswali yake yapate majibu au kumezwa na matendo yake ya imani na matumaini aliyokuwa nayo, kwa mfano pale chini ya msalaba aliposulibishwa mwanaye.  Tukio hili la kubaki hekaluni linaendelea kidogo baada ya kurudi Nazareti.  Kwa miaka kumi na nane ya thamani kuu inayofuata katika maisha yake, Yesu hakima anatenda jambo muhimu sana: anajifunza Maandiko Matakatifu ya Mapokeo yake ya Kiyahudi.  Je, anamsaidia Yusufu katika karakana yake ya useremala?  Anajifunza na kutenda matendo ya kibinadamu ya kupenda na kuchukia, ya kusaidia na kutelekeza watu?  Hapa tunaalikwa kuwa macho tu tukiangalia na kutunza mambo moyoni, kama ilivyombidi kukutenda mama yake.  Mengi yalikuwa bado mafumbo kwa Mariamu na Yesu kadhalika.  Anajiandaa kwa kuwa mwaminifu kwa muda, na muda unavyosonga mbele anajifunza kumwamini na kumtegemea baba yake wa Mbinguni.

Juma hili, tunakubali kushangaa, kuvurugikiwa na kuulizwa maswali kuwe sehemu tutakaposimama kuyatazama maisha ya awali ya Yesu Kristu.  Tunasali kwa kutumia hisia zinazoamshwa kwa kuuliza maswali magumu na hata kwa kutilia shaka.  Jinsi Yesu anavyokuwa bayana zaidi kwetu, sisi sura halisi ya nafsi zetu inakuwa bayana katika fumbo la maisha yetu ya kawaida.  Tunaanza kumwacha awe karibu nasi kila mmoja katika hali yake binafsi, na sote kama jumuiya moja ya binadamu. Neno limesemwa kwanza katika Mji wa Daudi na sasa kwa ajii ya wote kila mahali katika dunia ya Mungu.

Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...

Yesu Mpendwa,

Kwa namna fulani nimekuwa nikikuwaza wewe kama mtu mzima tangu awali yako ya kuwa mtu kama sisi.  Sasa naona wazi kuwa ulipitia utoto, ila mara Injili inakuelezea ukiondoka nyumbani kama mtu mzima.  Kulikuwa na nini katika miaka kati ya utoto wako na utu uzima wako?  Kulitokea nini baada ya wewe kutoka katika banda la ng’ombe ulipozaliwa kule Betlehemu na wazazi wako kwenda nawe nyumbani?

Ningependa sana kujua zaidi jinsi ulivyokuwa utotoni.  Ulipoanza kutembea, ulikuwa uliyechekesha watu kwa jinsi ulivyoitumia miguu yako kwa mara ya kwanza na kupenda kuendelea kujidhatiti kutembea hata ilipoonekana wazi kuwa ulikuwa umechoka? Sijaona popote palipoandikwa kukuhusu wewe ulipokuwa na umri wa miaka miwili, ila inanifurahisha ninapokufikiria kama mtoto wa miaka miwili mchangamfu na mwenye furaha, unayetaka kuchunguza mambo, kutaka kufikia na kuchukua kila ulichokiona, ukikwea kila ulipoweza hata pale ambapo hukupaswa kwenda, ukipita kati ya miguu ya Yusufu anapofanya kazi katika karakana yake ya useremala, ukicheza jikoni Mariamu alipokuwa akipika...  Napenda kukuona wewe ukiwa katika namna hiyo, kwa kuwa hapo utu wako ulio kama wangu unaonekana zaidi; na kuwa ni kwa namna kama hii sote tulijifunza mengi tulipokuwa tukikua kama watu wenye maswali na udadisi mwingi kuhusu maisha na watu wengine waliokuwa nasi katika maisha.

Ulijifunza vipi kusoma?  Mariamu ndiye aliyeketi nawe na kuanza kukufundisha Maandiko Matakatifu?  Yusufu ndiye alikuchukua kwenda na wanaume katika sinagogi? Rafiki uliocheza nao walikuwaje?  Ni nini ulichojifunza kuhusu ulimwengu ulipowatazama wafanyabiashara katika soko, ulipokutana na majirani, ulipoonana na wateja wa Yusufu, ulipokuwa na ndugu zako?

Bila shaka Yusufu alikuwa na ushawishi mkubwa sana katika maisha yako, na mara nyingi ulisimama karibu naye alipofanya biashara na wachuuzi.  Alikuwa mtaratibu na mwaminifu ila mwenye nguvu katika msimamo wake.  Mara kadhaa alikwenda sokoni kumsaidia mjane jirani kwa kuwa wachuuzi daima walijaribu kumlanghai na kumpunja.  Ulimtazama Yusufu akizungumza nao, akisisitizia haki ila kamwe hakuwai kujaribu kupata zaidi ya kile kilichostahii.

Ninavyoiona nafsi yako ya kuvutia, bila shaka ulikuwa mmojawapo wa viongozi wa wavulana katika mtaa wako, mkikimbia huku na kule hapo mjini na kurudi mkicheka na kufanyiana mzaha hadi katika karakana ya Yusufu.  Mara moja ulihadaa katika mashindano yenu ya kukimbia, na Mariamu alikuona ukifanya hivyo.  Alikuita pembeni na kwa taratibu alikusimulia hadithi ya fumbo yenye kuonyesha ubaya wa kuhadaa, na mara ndani moyoni uliwaka kwa majuto.  Kusahihishwa kwa utaratibu namna hii ndiko ulikokuhitaji kukusaidia kurudi kwa wenzako ukiwa umesonga mbele zaidi katika unyofu wa moyo na uwajibikaji kama kiongozi mmojawapo wa wavulana wenzako.

Ulipokuwa na miaka kumi na miwili, ulikuwa na safari muhimu na sana kwenda Yerusalemu ukiwa pamoja na kundi kubwa la watu wa familia yako na marafiki kutoka Nazareti.  Ulipofikahapo ulichungulia ndani ya hekalu na kuvutiwa sana na yale yaliyokuwa yakijadiliwa hapo.  Ulitaka kubaki na kutazama yote, ila marafiki zako walikuvuta, na mara mlianza kukimbia huku na kule katika mitaa ya Yerusalemu.  Najua ulishangazwa na lile soko kubwa sana karibu na hekalu, ambapo pia bidhaa kutoka nchi mbalimbali ziliuzwa.  Uliwaangalia kwa mvuto wa pekee watu wa namna mbalimbali katika jiji hili—walikuwa tofauti sana na watu kutoka katika mji mdogo ulipoishi.

Lakini kwa ukimya ulijitenga na marafiki zako, nguvu ya kile ulichokiona hekaluni na Yule aliyekuwa akijadiliwa ilikuvutia kurudi hekaluni.  Lakini, ee Yesu, haukufikiri chochote kuhusu wazazi wako?  Mara nyingine nashangazwa na jinsi ulivyokuwa hekaluni.  Cha kwanza, ulikuwa mvulana mdogo wa miaka kumi na miwili tu—hakudhani ukweli huu ulipaswa uuzingatie?  Mariamu na Yusufu waliogopa na kutaabika sana walipogundua kuwa haukuwa nao katika safari ya kurudi Nazareti.  Ila waliliwazwa sana walipokupata.  Ninapojaribu kutafakari lililotokea hapo na baada ya hapo, ee Yesu, nadhani ulipofika nyumbani walikuadhibu kwa kukukataza kwenda kucheza kwa juma zima.

Lakini ulikuwa mtoto mwema na hali ya wazazi wako kwako iliyoonyesha kupendelea nidhamu, upendo, imani na haki, vilisaidia kukulea kuwa ulivyo; vikisaidiana na mafunzo ya Mariamu, na bidii ya Yusufu katika kazi 1uliyoona na kuitamani kila siku.

Najisikia karibu nawe ninaposali nikikuona taratibu ukikua kuelekea ukomavu wa mtu mzima.  Hata hivyo bado najihisi napenda kukujua zaidi.  Ni lini ulipata ufahamu kuwa una mwito wa pekee kutoka kwa Mungu?  Ulianzaje kuwa mtumishi wa wengine, mwoshaji wa miguu ya watu?

Mpendwa Yesu, nisaidie kukuelewa zaidi ili niweze kufanana nawe zaidi.  Nisaidie kutafuta namna ambayo naweza kumtumikia Mungu kama ulivyofanya.  Natamani kuwa nawe katika ulimwengu huu na kutumikia kama wewe.

Maandiko Matakatifu

Luka             2:22-38

Luka             2:39-40

Luka             2:41-52

Waebrania    1:1-2