JUMA LA NANE
Upendo wa Mungu Kwetu — Huruma Yenye Msamaha
Mwongozo: Vipi Mungu Sharti Afurahie

Katika juma hili tutazungukia upendo wa Mungu kwetu.  Tunataka kuuonja na kufurahia kikamilifu msamaha wa dhambi ambao ni zawadi ya Mungu kwetu.

Japokuwa tumejaribu kufunga kila tafakari ya udhambi wetu kwa uhalisi au ukweli wa huruma ya Mungu, juma hili tutajaribu kutoa nafasi kwa huruma ya Mungu iliyo chanzo cha msamaha wa dhambi iwe ‘kibwagizo’ cha yote katika juma zima.

Tunaanza kwa kumgeuzia macho Mungu.  Taswira ya Mama akimpakata binti yake yaweza kutupa motisha kubaki tukitazama uso wa Mungu.  Uso wa mama huyu utatusaidia kuanza kutafakari nguvu itokanayo na jinsi Mungu anavyotukumbatia.

Ninapoamka kuanza shughuli za kila siku, naweza kwa muda mfupi kujiweka mbele ya Mungu, mbele ya jinsi Mungu anavyonifurahia.  Ni kwa jinsi gani Mungu sharti afurahie utambuzi wangu wa jinsi anavyonipenda na kunisamehe! Kila siku, naweza kujikumbusha matukio mbalimbali ambayo yanaivuta roho yangu kuupokea undani wa msamaha wa pendo la Mungu.

Naweza kuwaza kuhusu furaha niliyopata pale mpendwa wangu aliyekuwa mgonjwa, waganga wakadhani ni kansa inayoua haraka na kwa maumivu makali, ila vipimo vikaonyesha haikuwa kansa.  Ninaweza pia kuwaza kuhusu furaha niliyopata pamoja na wanandoa marafiki zangu ambao kwa muda mrefu hawakupata mtoto yeyote, na baada ya miaka mingi ya kusubiri walipata mtoto.  Ni jinsi gani basi Mungu anatufurahia juma hili!

Tunapingana na kushawishika kuwaza jinsi Mungu awezavyo kutusamehe dhambi zetu au mienendo yetu miovu inayojumuisha yote tuliyopaswa kutenda lakini hatukuyatenda na yote tuliyopaswa kutokuyatenda tukayatenda, huku tukiwa tunajua kuwa haikuwa sawa wala halali.  Ukweli kuhusu namna hiyo atutendeavyo Mungu ipo katika fumbo la upendo wake kwetu, upendo usio na masharti wala kikomo.  Tunaweza kuwaza kuhusu kumsamehe mwenzi wa ndoa au mtoto au yeyote tumpendaye si kwa sababu nyingine zaidi ya kuwa upendo tulionao kwake ni mkubwa na wenye nguvu kuliko mabaya aliyotutendea.  Hapa naweza kujiambia ni jinsi gani basi upendo wa Mungu kwangu ni mkuu: kunisamehe mimi kwa uhuru kamili na kwa ukamilifu hakika upendo wake ni mkubwa kupita hata uwezo wangu wa kuuwaza.

Upendo wa Mungu kwetu ni mkuu hata wakati mwingine tunajikuta tunashawishika kutokuuamini, ila tunashindwa na ukweli ulio dhahiri mbele ya macho yetu na hitoria yetu.  Juma hili tunawaza sio tu kuhusu kishawishi cha kutokuiamini huruma ya Mungu ituleteayo msamaha, bali pia tunasonga mbele kuishuhudia katika maisha yetu wenyewe, kuikubali na kuifurahia.  Hakika tutakalo kufanya juma hili ni mapenzi ya Mungu kwa kila mmoja wetu.

Tumia zana utakazopewa hapa mbele kurutubisha na kustawisha mafungo yako katika juma hili.  Utapata zana nyingine zaidi katika Mtandao wa mafungo haya.  Jaribu kuchangia neema upatazo juma hili na wengine kwa kupitia katika mtandao huu.  Hatuwezi kujua thamani ya zawadi ya neema tunazopata inaweza kuwa ya msaada kiasi gani kwa wenzetu pale tunapowashirikisha wengine katika mtandao huu.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili
Juma hili si rahisi kwa wengi.  Katika kufundisha kuhusu huruma ya Mungu kwa wale viongozi wa dini wanaomkosoa Yesu katika kula na kunywa kwake na wadhambi (Luka 15), Yesu anatoa mifano kadhaa yenye mafundisho, mmojawapo ukiwa mfano tuujuao kama wa “Mwana Mpotevu”.  Katika mfano huo, mwana mdogo anarudi akiwa amejawa na moyo wa toba kwa babaye: “Baba, nimemkosea Mungu, na nimekukosea wewe pia. Sistahili hata kuitwa mwanao.”  Yule mwana mkubwa anajawa na hasira na anaudhika sana kuwa baba kamsamehe yule mwana mdogo kirahisi hivyo.  Kama vile wale viongozi wa dini wanaomkosoa Yesu, huyu mwana mkubwa anakataa kuungana na babaye katika kusherehekea kurudi nyumbani kwa nduguye.  Si rahisi kwetu kuzishinda hisia za kutisha kuhusiana na dhambi na mienendo ya dhambi na uovu katika maisha yetu.  Hata pale tunapopata Msamaha wa Dhambi utokanao na upendo wa Mungu, daima tunakuta ipo sauti ya kaka au dada yetu mkubwa ndani yetu ambayo inadharau, inakasirishwa na kukosoa kusherehekea kwetu upendo, huruma na msamaha tuliopokea.

Juma hili ni la kujikabidhi kikamilifu katika mikono ya Mungu.  Mwone Mungu kama Baba anayekukumbatia kwa upendo na huruma, bila kujali hali ya uchafu wa udhambi wako.  Irudie picha hii yako na Mungu.  Baki hapo katika mikono yake ukifurahia tabasamu lake la upendo.  Usiwe na haraka ya kuondoka mikononi mwake.  Usiwe na haraka: baki hapo hadi woga wako wote uyeyuke kwa kujazwa imani kuwa upendo wake hauna mwisho.  Pokea upendo huo na kuuacha uwe kiburudisho cha moyo wako.  Jaribu pia kufikiri na kujiuliza: Je huyu Baba anayenikumbatia anahisi nini na anapenda mimi nijisikieje hapa katika kuungana nami kwa kunikumbatia kwa upendo?

Hili ni juma la kutabasamu — kutembea daima na tabasamu usoni mwetu na pia kulihisi ndani kabisa mioyoni mwetu.  Tabasamu na pumzi nzuri huenda pamoja barabara.  Kwa pamoja hufungua njia ya kuelekea kwenye furaha na amani iburudishayo na kuhuisha moyo.  Je, hii ina maana kuwa matatizo yangu yote yataniondokea?  Maisha yangu yatakuwa tena katika mkondo onaofaa?  Nimefikia upeo wa uhuru wa kiroho?  Bila shaka sivyo.  Tunaendelea kujikumbusha kuwa hii ni safari, na kila juma ni hatua muhimu itusongeshayo mbele.  Juma hili ni hatua yenye umuhimu wa pekee: kushuhudia, kuburudika, kufurahia na kusherehekea ukweli kwamba mimi ni mdhambi ninayependwa bila kikomo.

Labda juma hili naweza kupata vitu kadhaa vya kutenda ambavyo vitanigusa moyoni na kuchangia kulifanya juma hili liwe hasa la burudani na amani.  Lipange juma hili; fanya mabadiliko katika ratiba yako ya kila siku ili kulifanya juma hili likupe hisia tofauti.  Cha maana kupita yote ni kuwa juma hili linahusu kuwa na moyo wa shukrani na kuitoa hiyo shukrani.  Nahisi nini ninapokuwa katika mikono ya Mungu anayenikumbatia kwa mapendo?  Baada ya yote niliyotenda na wajibu ambao sikutimiza, na nikiwaza mienendo isiyo mizuri ambayo bado ni sehemu ya maisha yangu, najawa na mshangao wa kusamehewa kikamilifu!  Hisia gani zinanijia?  Kama machozi yananijia machoni, nayaacha yashuke usoni.  Nitamrudishia nini huyu anayenipenda kiasi hiki?  Hakuna chochote kitakachotosheleza.  Najaribu tu kutoa maneno machache ya shukrani.  Hakika kusamehewa ni zawadi kubwa na ya pekee.  Tunataka kutoa shukrani zetu kwa maneno ambayo yanaipokea zawadi hii na kutuwezesha kukaa ndani ya furaha na amani inayoletwa na msamaha huu.  Hapa matendo ya kiibada ni muhimu.

Matendo ya kiibada huhusisha miili yetu na hivyo kutuachia kumbukumbu ya kudumu.  Labda naweza kuandika maneno ya shukrani yangu katika karatasi, nikielezea jinsi ninavyojisikia — maneno haya nikiyafanya kama barua ninayomwandikia Yesu au Mungu moja kwa moja.  Nitakapofikia sehemu isomekayo: “Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...,” ninaweza kutumia maneno yangu mwenyewe, nikiyasema kwa sauti, kimoyomoyo au kuyaweka katika maandishi.  Baadhi yetu kuwa katika ukimya wa vyumba vyetu, mikono ikiwa imeelekenzwa mbinguni ni namna nzuri nzuri na tosha zaidi ya kuonyesha mbele za Mungu jinsi tunavyojisikia.  Kwa baadhi yetu, inakuwa vizuri na kuleta maana zaidi kuchagua au kutunga wimbo wenye maana inayolingana na hisia zetu na kuuimba mara kadhaa kwa mdomo utamkayo yatokayo mioyoni mwetu.  Labda pia naweza kusherehekea Ibada ya Ekaristi takatifu katikati ya Juma au Jumapili, au pia naweza kushiriki katika Ibada ya Jumuiya au Kanisa ninaloshiriki nikiwa nimejawa na hisia za furaha kubwa.

Kipimo kizuri cha maendeleo yetu juma hili ni jinsi tunavyolala kila siku.  Kama ninakwenda kulala nikiwa nimejawa furaha moyoni, na ninavyoaka pia naamka nikiwa na furaha moyoni kwa sababu ya ukweli kuwa mimi ni mdhambi ila napendwa kupita jinsi wengi wanavyoweza kuamini — basi neema ya juma hili itajaza amani roho yangu.

Kwa Ajili ya Safari: Kujifunza Kutembea Katika Njia ya Mungu
Juma hili tunasherehekea huruma ya Mungu kwetu na kwa ulimwengu wote.  Mlio au mliopata kuwa wazazi au mababu au wajomba au shangazi mmewahi kuwa na nafasi ya kuwahimiza watoto kuanza kutembea.  Unasisimka kwa furaha pale wanapochukua hatua ya kwanza na unajikuta ukicheka pale anapoangua kwa kishindo.
Hapa mtoto aweza kutaka kulia na kukuangalia jinsi unavyoipokea hali yake.  Tabasamu lako, mikono yako uielekezavyo kwake, jinsi unavyomgusa taratibu huwa mwanzo wa kuamka kwake ili achukue hatua nyingine.
Ni nini kingetokea iwapo ungeonyesha hasira na kukatishwa tamaa kwa kuwa mtoto kashindwa kuchukua hatua ya pili?  Mtoto atakuwa na mtazamo hasi wa nafsi, atajiona yeye si lolote, na kunyanyuka kwake ili kuendelea kunaweza kuwa taratibu, au hata anaweza asinyanyuke akabaki hapo chini.

Huruma  ya Mungu ni zaidi ya msamaha kwetu.  Huruma ya Mungu pia hutuwezesha kusimama tunapoanguka pale tujapojifunza kutembea katika njia ya Mungu.  Huruma si tendo la kisheria kama vile uamuzi wa mahakama.  Huruma ya Mungu ni ishara hai ya kimahusiano ibubujikayo kutoka katika kiini cha upendo wa Mungu.  Ni kwa upendo huu huu alituumba sisi kwa sura na mfano wake, na ni kwa upendo huu anazidi kutupa uhai.

Pale Yesu anamwonea huruma mtu au makutano ya watu, maana yake hasa si kwamba anawasikitia au anawasamehe.  Yesu anaonyeshwa kama anayeguswa kutoka ndani kabisa, kama vile kutoka tumboni ambapo hisia zilidhaniwa kuwa ndipo zilipokaa.  Yesu anavutwa kunyoosha mkono wa msaada, kuwafundisha, kuwalisha, na kuwaongoza wanadamu wenzake waliopotea na kuanguka.

Kusali katika juma hili ni kwa ajili ya kutufanya huru tusimwogope Mungu ambaye kwa upotovu tulimwona kama hakimu mkali au mzazi aliyekatishwa tamaa na kuanguka kwetu zaidi ya mara moja.  Tunaalikwa kupokea mguso tulivu wa Mungu na kuhimizwa kusimama na kuendelea kujifunza jinsi ya kuwa mfuasi wa Mungu.

Huruma ya Mungu ina nguvu zaidi ya kazi zote za Mungu, na hii ni bayana katika kumtoa Mwanaye awe binadamu kama sisi ili kutuonyesha njia ya kumwendea Mungu Muumba wetu.  Tukiwa na utambuzi wa huruma hii ya kumwacha Yesu awe Yesu, yeye atukomboaye, tunasali bila woga kwa Mungu mwenye huruma hii ya ajabu kwetu.
Hivyo basi tunaanza juma hili kwa kusherehekea utakatifu wetu ambao unahusisha ukweli wa uhitaji wetu wa huruma na upendo wa Mungu utuhuishao na kutupa nguvu.  Huruma au rehema hii, inapopokelewa kwa shukrani, hatimaye itatuweka huru kwa ajili ya kazi muhimu zaidi ya kutembea katika imani kuelekea pale Mungu atakapokuwa nasi daima.  Tunasali taratibu tukijawa na utambuzi wa kiimani kuwa Yesu alikuja kutuokoa na siyo kututatua.

Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...
Bwana Mpendwa,
Tazama sioni maana yoyote... Ni vipi naweza kuziangalia dhambi zangu nyuma yangu, maanguko yangu na makosa yangu na bado nabaki na utambuzi mkubwa wa wa upendo wako kwangu?  Hauchoshwi na kushindwa kwangu mara nyingi sana katika kukupenda wewe na wengine kama utakavyo?

Na hapa naiona maana hasa: upendo na huruma yako!  Ninayo taswira ya mwana mpotevu akiwa njiani kuelekea kwa babaye, akiwa kapungukiwa nguvu kwa kukosa chakula lakini anasonga mbele akichechemea, huku arudiarudia maneno atakayotumia kuomba msamaha wa baba yake.  Akiwa na fadhaa na wasiwasi ghafla anamwona baba yake akikimbia kumwelekea akiwa na mikono wazi tayari kumkumbatia kwa furaha.  Kinachonishangaza na kunigusa ndani sana ni furaha ya baba anapokimbia katika uzee wake kumwelekea mwenaye.  Naiihisi furaha yako ndani yangu unaponikaribisha na kunichukua mikononi mwako.  Naona wazi kuwa umekuwa barabarani kila usiku na pendo kuu moyoni, ukingojea bila kuchoka kurudi kwangu.

Hii ni hisia nzuri sana!  Najua nilianza kwa kusema kuwa sikuona maana yoyote, ila hiyo ni kwa sababu nilikuwaza wewe kuwa mwenye upendo ulio hafifu na wenye kikomo kama wangu.  Sasa naona jinsi upendo wako usivyo na mipaka wala kikomo.  Asante sana kwa upendo wako huo unizungukao pande zote naweza kuufurahia, kuusherehekea na kujisikia mwenye amani na usalama wa hali ya juu.

Nisaidie, ee Mungu wangu, kuenenda na pendo hili juma hili lote.  Nisaidie kuwa na imani makini juu ya upendo huu, nisisikilize sauti ndani yangu ambayo inaniambia kuwa mimi si lolote wala sistahili kupendwa nawe.

Acha nitulie kimya ndani ya upendo huu; niuhisi ukiingia na kuupenya kabisa ya moyo wangu.  Niache nipokee upendo wako, na kuuruhusu unizunguke pande zote, kuniweka salama na kunijaza amani yako, nisiogope lolote kamwe.  Nashukuru sana Bwana kwa zawadi hii.  Najua siistahili, na ukweli huu unaifanya zawadi hii kuwa yenye thamani kubwa zaidi kwangu.  Upendo wako kwangu ni mkubwa sana na unapenya sehemu zote za maisha yangu japokuwa unajua kikamilifu jinsi gani mimi ni mdhaifu na mdhambi.

Asante sana Bwana wangu kwa zawadi hii ya msamaha na upendo.  Nijalie wiki hii niishi nikiwa na utambuzi wa upendo wako binafsi kwangu.

Maandiko Matakatifu:
Yohana 4:5–42
Yohana 9:1–4
Yohana 8:3–11
Hosea 14:1–10
Luka 15:11–32

MAFUNGO YA KIROHO KUPITIA MTANDAO