JUMA LA KUMI NA TANO

Kazaliwa Kwetu, Kwa Ajili Yetu

Mwongozo: Neema ya Kuzaliwa Kwake

Akinamama wengi, katika kusherehekea siku ya kuzaliwa ya watoto wao, huwasimulia kwa kwa uyakinifu yaliyotokea siku na wakati walipozaliwa.  Mwaka hadi mwaka, simulizi hizi hurudiwa. Katika muda huu wa mafungo yako, tunampa Yesu nafasi atupe simulizi ya kuzaliwa kwake.  Hii itatubidi twende mbele zaidi ya simulizi tunazopata katika Injili kama zilivyoandikwa na Matayo na Luka.  Tutaingia ndani kabisa ya simulizi kuliko tafakari zetu za kuzaliwa kwa Yesu Kristu.  Juma hili tutapokea neema ya kushuhudia kuzaliwa kwa Yesu na kuelewa maana yake hasa na umuhimu wake kwetu.

Uchu wetu unaendelea.  Ni lazima kwetu kuiamsha upya kiu hii ndani yetu katika juma hili, (iwapo imefifia)—kiu au uchu wa kumjua Yesu kwa undani zaidi.  Kwa kumwangalia na kumwelewa, tunategemea upendo wetu kwake kuwa mkamilifu zaidi.  Upendo wetu kwake unavyoongezeka katika ukamilifu, tunapata uhiari mkubwa zaidi wa kuwa naye katika utume wake.

Kwa hiyo, tutakachozingatia akilini mwetu na katika yote tuyatendayo katika juma hili la mafungo ni pote, yote, wote na vyote, vilivyokuwepo na kutokea katika kuzaliwa kwa Yesu.  Hii itatuelimisha Yesu ni nani.  Hata hivyo, kama tulivyoshuhudia hapo awali, kujua huku hatukupati kwa zoezi la kitaaluma, bali zoezi la kushiriki, hivyo basi kuwa mtendaji au mshiriki katika tukio lenyewe. Tunahitaji kupitia matukio yaliyojiri ili kuona wasiwasi uliochanganyika na hamasa waliyokuwa nayo wazazi wake, hali ya ufukara waliyokuwa nayo; na kwa upande mwingine amani na kuridhika kwao kuwa katika hali hii ambapo ajabu ya kuzaliwa kwa Yesu kama mwanadamu kamili inawaletea furaha; Tunaona pia ajabu ya kutembelewa na wachungaji, na mambo ya hatari ambayo yanaanza kujitokeza kuhatarisha maisha yake.

Je, wiki hii naweza kuupa nafasi kila wasiwasi ninaouhisi uunganike na wasiwasi wa Mariamu na Yusufu?  Ninaweza kushirikishwa katika uchungu wa uzazi aliokuwa nao Mariamu katika kujidhatiti kuwa mkarimu kujitolea kusaidia wengine ili waishi?  Naweza kutambua vitanda vya ambapo ninasihiwa kujilaza kwa furaha? Na naweza kuona vitanda hivi vikibadilika ninapomwangalia Mtoto Yesu akiwa amelazwa katika kitanda cha yasi horini?  Wapo watu maskini au walemavu au wowote wanaotaabika ninaokuwa nao au kukutana nao maishani ambao wananikumbusha jinsi gani wachungaji walikuwa na furaha sana walipokaribishwa kushuhudia ukweli wa kuzaliwa kwa Yesu?

Katika juma hili itahidi kuwa mshiriki katika matukio yanayosimuliwa uyaelewe kwa kutumia hisia zako hai.  Jaribu kuwashirikiwa wengine neema unazopokea katika ukurasa: Sehemu ya Kuchangia na Kushirikishana katika mtandao huu.

Yesu Kristu aliyeingia katika maisha yetu katika ukamilifu wa hali yetu ya kibinadamu na azidi kutusaidia kukua katika kumjua na kumpenda wakati huu.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili

Kutafakari kuzaliwa kwa Yesu kunaweza kuwa tendo la kufurahisha sana.  Zaidi ya hayo, kufanya tafakari hii katika mazingira ya maisha yetu ya kawaida kunaweza kuwa chanzo cha nguvu ya kipekee.  Katika usaidizi wa sala juma lililopita tulipata maelekezo ya msingi katika kutafakari Maandiko matakatifu wakati wa sala, katika hali maalum ya mafungo haya.

Tumezoea sana kusikia simulizi za Krisimasi (Noeli), na kichwani tuna picha nyingi za siku hiyo ya kuzaliwa kwa Yesu Kristu. Juma hili na tupenye ndani zaidi ya simulizi ya Noeli kwa kuwa ndani kabisa ya yale yaliyotokea siku hiyo; tuingie si katika simulizi tu, bali katika ukweli wa kuzaliwa kwa Kristu, na jinsi ukweli huu unavyotuambia Yesu ni nani.

Kila asubuhi niamkapo, nitawaza ni kipi napendelea kiwe katika mawazo na kumbukumbu zangu siku nzima.  Katika siku za kwanza za juma, naweza kufanya matayarisho ya jukwaa. Katikati ya juma, naweza kushuhudia kuzaliwa kwa Yesu.  Baadaye katika juma, naweza kutenga muda wa kuwa na Mariamu, Yusufu, Mtoto Yesu na wachungaji wa kondoo.  Naweza kufunga wiki kwa kuipitia upya simulizi ya kuzaliwa kwa Yesu kama ilivyoandikwa katika Injili ya Matayo, uhasama wa Herodi, wahujaji kutoka Mashariki na familia takatifu kukimbilia Misri ili kuokoa maisha ya mtoto.

Kama tukipanga vipindi vya sala katika juma hili na kuvifuata ipasavyo, itakuwa rahisi kuingia katika matukio husika na kuyatafakari ipasavyo.

Naweza, kwa mfano, kujitafakari kama rafiki wa Mariamu na Yusufu.  Naweza kuwatembelea mara nyingi wakati Mariamu akiwa mjamzito, na kufurahia kumwona Mariamu akimwimbia Zuburi mtoto wake, ambaye anasikiliza angali tumboni.  Nasikiliza mazungumzo kati ya Yusufu na Mariamu—mazungumzo yenye ujazo mkuu wa imani kwa Mungu. Namwona Mariamu akipapasa tumbo lake, kama vile kumtuliza mtoto tumboni mwake kwa imani yeke.  Nahisi furaha kubwa pale Mariamu anaposhika mkono wangu na kuugusisha katika tumbo lake, na nahijisi kuwa karibu sana na mtoto anayekua tumboni mwa Mariamu.  Naweza kuwashukuru Mariamu na Yusufu kwa uwazi wao na “ndiyo” yao kwa Mungu.  Naweza kutoa shukrani zangu kwa ajili ya kunishirikisha imani yao na furaha waliyonayo kwa ajili ya mtoto wao, na pia kwa kunipa nafasi ya upendeleo kushuhudia na kuwa mwandani wa familia hii katika hali hii ya mwanzo.  Naweza kuwaambia lolote ninalotaka kuhusu maisha yangu na yale yanayonikabili leo hii.  Katika sehemu hii niliyofikia katika mafungo haya, Mariamu na Yusufu wanaweza kuwa marafiki wangu wakubwa katika safari ya maisha yangu.  Labda nitakuwa nao hapo habari kuhusu sensa inapowafikia.  Wanaukabili vipi wasiwasi wao? Naweza kukumbuka maneno halisi waliyosemezana?

Ninapowasindikiza katika safari yao kwenda Betlehemu kuhesabiwa, ninaionaje safari hii?  Barabara, uchovu, woga, mazungumzo yao: yote nayashuhudia na kuwa sehemu yake kwa kiasi fulani.  Je wanalichukulia jambo hili tofauti na jinsi nilivyokabili changamoto kama hii katika maisha yangu?  Ni maneno gani ya kiimani mtoto Yesu anayasikia kutoka tumboni mwa mamaye katika safari hii?

Unaionaje hali yao wanapokosa nyumba ya kulala ugenini Betlehemu?  Mtoto anashuhudia nini katika maneno “Hapana, hakuna nafasi kwa ajili yako hapa,” “Hapana, haukaribishwi hapa”, na “Nyumba imejaa”? Naweza kukumbuka maneno yao hasa waliyoambiana wakitoka sehemu moja kwenda nyingine?  Ilikuwaje pale ilipobidi wajipatie pa kulala katika nyumba ya wanyama?  Tumia uwezo wako wa kufikiri na kutafakari, ukitumia milango yote ya fahamu.  Waliona uzuri wa mahali hapo? Walijua kuwa zizi la ng’ombe lilitosheleza nia yao, tena kwa ukamilifu?

Naweza kwenda karibu kiasi gani na pale anapozaliwa Yesu?  Naweza kwenda karibu kiasi ninavyotaka. Kama nimewahi kuwa na mtoto au kuona mtoto akizaliwa, naweza kutafakari jinsi Mariamu anavyoukaribisha uwepo wangu.  Ni maneno gani namwambia? Mariamu anapoingia katika uchungu wa uzazi, yeye na Yusufu wanaambiana nini? Wanazungumza na mtoto tumboni mwa mamaye?  Naweza kusogea karibu kiasi cha kuwa mshiriki katika tukio hili na kutambua maana yake?  Naweza kumpokea mtoto mchanga anapozaliwa mikononi mwangu?  Mwili wake vuguvugu akiwa na damu mwili mzima, anavuta pumzi na kutoa kilio huku akiyoosha mikono yake kulia na kushoto, kama vile kuukuumbatia ulimwengu.  Naweza kumfunika asihisi baridi na kumlaza manyasini katika hori la kulishia ng’ombe? Ndani moyoni, nahisi kuwa yote haya ni yangu; yote haya ni kwa ajili yangu?

Katika siku zinazofuata, tunaambiana nini?  Ninapotafakari kuwasili kwa wachungaji pale alipozaliwa mtoto Yesu wanapata mandhari ya namna gani?  Wanapoondoka, naweza kutafakari maneno ambayo Mariamu na Yusufu wanamwambia mtoto wao kuwa siku moja atajitolea maisha yake kuleta habari njema kwa maskini?

Kama tukifanya juhudi kupenyeza katika matukio haya kwa kutumia uwezo wetu wa tafakari hai, itakuwa rahisi kwetu kuendelea na shughuli na kazi zetu za kila siku tukiwa na picha hai za matukio haya mioyoni na akilini mwetu.  Matukio ya kila siku yatakuwa yakishabihiana na yale katika ya uzazi wa Yesu: woga na wasiwasi, imani, matarajio, safari, matatizo, vizingiti visivyotarajiwa, kukataliwa, kutokukaribishwa, kufanya mipango mbadala, umaskini, kitanda cha nyasi na kupokelewa kirahisi.  Siku nzima, naweza kuwa naona na kutambua na kufananisha mambo; huku nikiendelea na mazungumzo, kumbukumbu ya maneno na utambuzi wa hisia zangu.

Nipokwenda kupumzika kitandani mwisho wa siku, naweza kutoa shukrani zangu kwa yote niliyopata siku ya leo.  Naweza kumwambia Yesu ni kiasi gani ninatamani kuwa naye katika utume wake, kwa kuwa mapendo yangu kwake yanakuwa dhahiri zaidi anaponipa nafasi ya kumjua zaidi.

Kwa Ajili ya Safari: Unaona Nini?

Juma hili tunaangalia na kusikiliza simulizi zaidi ya Mungu mwenyezi kuwa kitoto kichanga.  Yote si tulivu na angavu pale Yusufu na Mariamu wanapoanza safari kwenda Betlehemu.  Kuna mwanga wa kutosha, ila hakuna utulivu katika nyumba ya wageni ambapo wanakosa nafasi.  Yote si angavu katika banda la wanyama ambapo wanapata nafasi, ila wanapata utulivu baada ya safari ndefu.

Tupo na Yusufu, mume ambaye hawezi kufanya yote anayohitaji mkewe wakati huu.  Tunamwona akihangaika kutenda hili na lile—akiwasha moto ingalao mtoto na mzazi wasipate baridi sana, na pia tunamwona akijitahidi kulisafisha zizi la ngombe ili lifae zaidi kuwa pango kwa familia yake hii changa.  Tunauhisi ukimya wa usiku, ukimya wa muda kama vile saa haisongi mbele.  Ukimya huu ni sauti ya yule Asiye na Kikomo cha Muda, ambaye ameingia katika ulimwengu wetu sisi tulio na kikomo cha muda.

Umeketi au umesimama wapi?  Unamwangalia nani kwa ukaribu?  Unavutiwa na hawa wanadamu wawili wakimstaajabia mwanadamu wa tatu ambaye sasa ametulia katika hori la kulishia Ng’ombe?  Unavutiwa kusogea karibu na walipo au unasukumwa kutoka nje?  Mariamu anakwambia chochote kwa maneno au kwa ishara?

Na sasa ukimya unaisha kwa kuwasili kwa wachungaji wa kondoo.  Wameuona mwanga, na kugutushwa na malaika waliokuwa wakiimba wimbo wa amani duniani.  Unavutiwa kuwaambia chochote kuhusu uliyojionea?  Je, hapo pamekuwa mahali pa kushangaza na penye mengi ya kutafakari? Mariamu ameketi hapo akishuhudia yote na kuyachanganua na kuyatunza moyoni.  Alikuwa kalisemea ndiyo fumbo hili alipoamini ahadi ya Mungu.  Tayari kashuhudia sehemu kubwa ya fumbo hilo usiku huu.  Maswali yote ya “Ni ni hiki hasa?”, “Kulikoni?” na “Itawezekanaje?” yanasukumana rohoni mwake; ukipenda unaweza kuketi karibu naye ukiwa na “ndiyo” yako uliyoitoa pamoja na “Nitendewe anavyotaka Mungu.”

Mtakatifu Inyasi anatusishi tuwe wawazi mbele ya Mungu, ili kwamba tuweze kupata neema ya kumshuhudia Mungu kwa uwazi anaopenda kutufunulia anapotuita.  Tunajua vema historia ya ukombozi wetu, ila kila tunaposali inakuwa zaidi na zaidi mali yetu na sehemu ya maisha yetu ya kila siku.  Hivi ndivyo Mungu anavyotueleza sisi ni nani na jinsi gani tupo katika mawazo yake na mpango wake.  Sehemu ngumu ya tafakari hii ni kuizoea.  Kwa kuwa watulivu, katika ukimya wa usiku huu, sala zetu zinaturudishia katika hali mpya ule mwangaza ambao wachungaji waliusikia: Leo hii, mtoto amezaliwa ambaye anatuletea amani ulimwenguni; Amani kwa wote wanaobarikiwa na Mungu; Amani kwa wote wenye mapenzi mema.  Amani, kwa Mtakatifu Inyasi, ni kwa wote ambao wanafurahia na kuburudishwa moyoni au kupata faraja kama matokeo ya tafakari zao za mafumbo matakatifu ya Mungu katika Neno lake, viumbe vyake au matendo yake tunayoyashuhudia kila siku katika maisha.

Tunamjia tena huyu mama mjamzito na mtoto wake atakayejifungua.  Tunasogea karibu naye au tunakaa kwa umbali kidogo kwa kadiri tunavyotaka.  Tunasali tukiwa katika hali ya uwazi kama vile mabanda tupu ya wanyama yanayongojea ukimya na mwangaza mpya uyajie na kuyabariki.

Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...

Yesu Mpendwa,

Nadhani ni harufu mbaya muozo wa nyasi za kulishia ng’ombe ndio unaonifika kwa uzito zaidi.  Najikuta nimesimama kwenye baridi nje ya zizi la ng’ombe, nikichungulia ndani kupitia ufa mkubwa katika zizi hilo.  Kuna mwanga hafifu ndani, ila unanitosha kuona yote yanayotokea ndani ya zizi.

Sala hii imekuwa safari ya kufurahisha na kusisimua.  Safari hii imekuwa sala ya kufurahisha na kusisimua. Niliwatazama Yusufu na Mariamu wakisafiri kwenda Betlehemu.  Mariamu alikuwa amekwishasaidia wengi waliozalia majumbani, lakini kwa sasa wakati wake unapokaribia hakuna mwanamke yeyote aliyenaye na anakuwa na woga kiasi.  Hakuwa amepata muda wa kumjua Yusufu kwa undani, ila alimpenda na kumwamini. Kwa miezi kadhaa, walikuwa wameshirikishana yaliyokuwa katika mioyo yao hasa walipozungumza kuhusu ujauzito wake, wasiwasi wa Yusufu, imani yao kwa Mungu isiyotetereka, na uamuzi wa Yusufu kuwa na Mariamu kuendelea na Mariamu katika ndoa na kuwa naye katika yote.  Yote hayo yalifanya kukomaa kwa muungano wao na kuwa na nguvu zaidi kuliko uletwao na mapenzi ya wawili walioana hivi karibuni.

Sasa ninaposali nikitafakari tukio la uzazi wa Yesu, nakutana nao katika zizi la ng’ombe na harufu isiyo nzuri ya nyasi za kulisha ng’ombe zilizooza ya kinyesi cha ng’ombe.  Inawezekanaje uzae mtoto hapa, katika nyasi za kulishia ng’ombe zenye uvundo uletao harufu mbaya? Inawezekanaje mwana huyu mtukufu azaliwe hapa katika zizi la ng’ombe ambapo kinyesi cha wanyama hawa kimetapakaa kila mahali?

Ninachotaka hasa ni kwenda katika lile zizi na kuwasaidia.  Nitaweza kweli?  Ee Yesu, naweza kusali kwa kutafakari na kuwa na hali ya kutojijali hata kuweza kuingia huko zizini?  Naingia na wote wawili wanaelekea kufurahia kuniona.  Mariamu ananikaribisha na kunishukuru kuwa nao hapo.  Yusufu amekuwa akishughulika kusafisha sehemu ambapo Mariamu angeweza ingalao kujilaza.  Anapoanza kupata uchungu mkubwa wa uzazi, namshika mkono kwa nguvu kumwashiria nipo hapo, nipo pamoja naye.  Lakini humu ndani kunanuka sana!  Ee Yesu, uliwezaje kuzaliwa sehemu panaponuka namna hiyo!  Nilianza kujaribu kuleta nyasi kavu ili kuzisambaza zifanye kirago kwa Mariamu, ila mara alianza kujifungua na ni mimi tu niliyeonekana kujali kuhusu nyasi kavu.

Ndipo ulipozaliwa katika nyasi tepetepe zilizonuka, na kupokelewa na mikono yenye nguvu ya Yusufu.  Alikupangusa uso na kusafisha pua yako na nacho na mara ulipotoa kilio kikali, wote walicheka.  Nami nilicheka pia kwa sauti ya chini, ila sikutaka kuwaingilia katika hali yao wakati huu walipoonekana wazi jisi walivyohusudiana, hivyo nilijiweka pembeni kidogo.  Ee Yesu, tazama moyo wangu unajazwa na uwepo wako!  Kuzaliwa kwa mtoto yeyote katika mahali kama hapa kunashangaza, sembuse wewe Muumba wa kila kitu. Pana baridi kali hapa, pananuka na hata hakuna kitanda wala blanketi kwa ajili yako kitoto?  Yusufu kakufunika kwa joho lake, ila naona unahitaji kufunikwa zaidi.

Sasa natambua uchovu mkubwa wa Mariamu na Yusufu baada ya safari ndefu, ila pia naona waziwazi jinsi wanafurahia sana kuzaliwa kwako usiku huu.  Mariamu anaposinzia akiwa kakubeba, anafumbua macho yake mara.  Naweza kukupakata wakati Mariamu na Yosefu wakiwa wamelala?  Ni ajabu sana kuaminika kiasi hiki!  Naketi taratibu katika nyasi ambapo sitakuwa nikiwasumbua, na nakupakata ukiwa umefunikwa joho la Yusufu.  Nakuangalia, nanusa shingo yako ya kitoto, nakupapasa mashavuni kama nilivyozoea kuwafanyia watoto wangu binafsi.  Nahisi upendo mwingi kwako na kwa yote ambayo umefanya.  Unakuja ulimwnguni katika hali kama hii—katika hali hii duni ndani ya zizi la ng’ombe linalonuka.  Unafanya haya yote ili kuwa nasi katika sehemu ya maisha yetu iliyo duni na yenye kunuka.

Yesu mpendwa, nijengee moyo wa unyenyekevu kama wako katika majuma ya mafungo yanayofuata.  Nipe uwezo wa kuhisi unyonge wako na kutambua unyonge wangu na kujisalimisha katika unyonge huo kama ulivyofanya.  Nisaidie niwe mdogo katika ulimwengu huu na kuwa hapa kwa ajili yako, japokuwa hii inashangaza kwa kuwa ni wewe uliye hapa kunisaidia.  Amina.

Maandiko Matakatifu:

Matayo            1:18-24

Luka                2:1-21

Matayo            2:1-12

Matayo            2:13-23

Zaburi              98

 

 

 

MAFUNGO YA KIROHO KUPITIA MTANDAO