JUMA LA MARUDIO

Kutua kwa Muda Ili Kukagua Neema Tulizopokea

Mwongozo: Kufanya Tathmini

Katika Mazoezi ya Kiroho, Mt. Inyasi anawasisitizia waongozi wa wale wanaofanya Mazoezi kuwakumbusha wanaofanya Mazoezi kuwa ni vema “kubaki” pale “wanapopata matunda.”  Majuma yaliyopita ya mafungo haya yamekuwa chanzo cha neema zenye nguvu.  Juma hili la marudio halianzi mada mpya.  Mada ya juma hili ni tafakari ya neema tulizopokea katika majuma kadhaa yaliyopita.

Baada ya kujijua kuwa sisi ni wadhambi tunaopendwa na Mungu, tulipata neema ya kualikwa kumfuasa Yesu.  Tunakumbuka miitikio yetu binafsi ya kumfuata, na kuongezeka kwa shauku ya kumjua na kuwa na Yeye aliyetupenda kiasi kikubwa sana.  Tumeanza kumpa nafasi atuelezee mpango wa Mungu na maisha yake. Tulishatafakari mwito wake na jinsi Mungu alivyotayarisha ujio wake kuanzia enzi za Agano katika Maandiko ya Wayahudi.  Kisha tuliingia katika simulizi za wazazi wake, na wale waliowazunguka katika maisha, wakati alipotujia kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.  Mwishowe tumejikuta tukiwa ndani ya banda la wanyama, pale anapozaliwa kwa ajili yetu.

Juma hili la mafungo tunakaribishwa kubaki hapo kwa muda kiasi.  Labda tumekuwa katika harakati nyingi sana kiasi cha kushindwa kukamata yote yaliyofunuliwa kwetu.  Yawezekana pia tunashindwa kuona kufanana kwa kuzaliwa kwake katika hali duni ya zizi la ng’ombe na kutujia katika umaskini wa maisha yetu.

Tunapoamka killa asubuhi juma hili, tutapitia tena neema fulani ambayo kwayo tunamshukuru Mungu.  Yaweze kuwa neema moja juma zima.  Yaweza kuwa kufanya jambo lisilo na vipengele vingi kama vile kufanya makazi yetu katika zizi lile la ng’ombe ili kuwa na Yesu mahali hapo.

Neema tunayotamani juma hili ni kuingizwa ndani zaidi katika nafsi ya Yesu Kristu. Juma hili tutapata misaada ya kuanza, ya kuingia ndani zaidi, na ya kutusaidia kupata maneno kwa ajili ya sala.

Tafakari zetu zitakuwa sehemu-fiche, lakini hai, katika kila linaloendelea katika maisha yetu kila siku juma hili.  Lolote tunalokabili kila siku katika wiki hii linaweza kuwa sehemu ya mafumbo ambayo tumekuwa tukitafakari, iwapo tutaliruhusu liwe.  Tukio lolote katika maisha ya mtu ni tukio ambalo Yesu Kristu amekuja kuwa sehemu yake.  Juma hili tunashuhudia upendo wa Mungu ukiingia ndani kabisa ya nyoyo na maisha yetu.

Mwishowe, kila jioni katika juma hili, tunatoa shukrani zetu kwa ajili ya neema mpya tunazopokea.  Kwa ingalao muda mfupi kila siku, labda tunapobadili mavazi ya kazi ili kupumzika kitandani, tunaweza kuinyanyua mioyo yetu kwa shukrani kwa Mungu kwa ajili ya misukumo ya kiroho siku hiyo—misukumo ambayo inayotuunganisha na Yesu ambaye amekuja katika ulimwengu wetu kuwa mmoja wetu katika ubinadamu, na kutukaribisha kujiunga na utume wake.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili

Kulianza juma hili sharti kwanza tujue wazi tofauti kati ya juma hili na majuma mengine yaliyotangulia.  Juma hili ni la kufanya marudio, kusita kidogo tulipofikia ili kupata muonjo kamili wa neema tulizopewa, au kuzipa nafasi zaidi zipenyeze katika sehemu zote za maisha yetu.  Hatufanyi mazoezi yote ya majuma yaliyopita, bali kuhakikisha tumepokea kwa ukamilifu zaidi neema za Mungu katika majuma yaliyopita kwa kuziona, kuzitambua, kuzipa majina na kuzipokea ziwe zetu zaidi au ziwe sehemu ya maisha yetu, kama Mungu anavyotaka.  Hivyo basi ni wazi kuwa hatufanyi marudio haya kwa kuwa hatutaki kuendelea mbele, na mtazamo wetu upo zaidi katika neema tulizopokea kuliko katika mazoezi tuliyopitia kuzipata neema hizo.  Hivyo basi, mfano mzuri tunaoweza kuutumia hapa sio wa kusoma kitabu kizuri, kisha kurudia kukisoma chote mara nyingine.  Mfano mzuri wa tunayofanya juma hili ni kama hivi: Rafiki yangu ananionyesha albamu ya picha za familia yake, na ananionyesha kwa kasi hasa kurasa za awali.  Namwambia rafiki yangu apunguze kasi ya kunionyesha picha na kumwambia: “Hakika picha hizi ni za kufurahisha.  Hebu tuuangalie tena ukurasa huu.  Nafurahia hasa kuziangalia picha hizi hapa kwa umakini zaidi.  Tazama jinsi baba na mama yako walivyokuwa vijana!  Na hii ni nyumba ambapo uliishi utotoni?  Tazama jinsi macho ya baba yako yalivyokuwa makali, labda hata sasa ni miwani yake tu inayaficha!  Na picha hii inaonyesha wazi jinsi ulivyo, japokuwa hapa ulikuwa bado kitoto kichanga.”

Kama tulivyoelezewa maana hasa ya marudio katika mafungo hapo juu, ni wazi kuwa njia nyingine ya kuelezea tunachofanya juma hili ni kwa upande wa sala za juma hili. Kama majuma mengine katika mafungo haya, juma hili tunasali, lakini siyo kwa kuchukua mada mpya za kusalia, bali kwa kutumia neema tulizopokea katika majuma yaliyopita.  Napokea neema niliyozawadiwa au nachukua neema niyokwishapokea na kuipenyeza kwa undani zaidi, kisha natulia ndani ya neema hiyo nikifaidi utamu wake.  Tunafanya hivi kwa kuwa tunajua kuwa daima kuna zawadi nyingine ndani ya zawadi tulizopokea.  Basi juma hili tutaziweka mbele yetu zawadi (neema) tulizopokea, na tutazifungua ili kugundua zawadi nyingine ndani ya hizi, ambazo pia tunakaribishwa tuzipokee ziwe zetu.

Hivi basi ni hatua muhimu ya kuonyesha moyo wa shukrani zaidi kwa zawadi tulizopokea—kujua hasa ni nyingi kiasi gani, thamani au umuhimu wake kwetu, na maana yake katika maisha yetu. Shukrani yetu haiwezi kuwa kamilifu ikiwa hatujui hasa ni nini tulichozawadiwa.  Hili ni zoezi muhimu sana kwa kuwa tunafanya mafungo haya katika hali ya kuendelea na shughuli zetu za kila siku, zenye changamoto zinazoweza kutufanya tusione na kupokea yote tunayopewa.  Iwapo neema za majuma yaliyopita, kwa mfano: mwito na mwitikio, ufahamu wa Mpango wa Mungu katika maisha yangu, utambuzi wa umwilisho wa Mungu kwa ajili yangu—zimekuwa zawadi katika maisha yangu halisi, basi zitakuwa na maana katika maisha yangu halisi:

  • Nimesema nataka kuwa na Yesu katika utume wake.  Leo nataka ingalao kuonja uchaguzi wangu huo katika kazi na yote nitakayochagua kutenda.
  • Nimetambua jinsi ambavyo Ujio wa Kristu ulikuwa mpango wa Mungu wa kutukomboa.  Leo nataka kwa makusudi na kwa ufahamu kamili kukubali kuwa katika mwili—hii ikiwa ni kupokea maajabu mengi ya mwili wa mwanadamu na pia mipaka, udhaifu wake na kudhoofika kunakoendana na kuwa nafsi-yenye-mwili.  Kuna nyakati katika siku ambapo nitaweza kuonyeshwa kwa uthabiti mimi ni nani hasa—mwenye mwili na nafsi niliyorithi; niliye na mambo kadhaa niliyochagua maishani; mwenye mwili wenye umbo na hali maalum: afya yangu, magonjwa yangu nk.
  • Nimeshuhudia na kuguswa moyoni na Kuzaliwa kwa Yesu.  Labda nimeingia katika zawadi ya tafakari hii ya jinsi Yesu alivyokuwa mmoja wetu.  Labda nimeingia katika matukio hayo na kumbukumbu ya matukio hayo ingali mpya au ngeni na bado inanipa misukumo ya ndani moyoni.  Leo hii nataka kutembea-tembea katika maisha yangu na kuona mivutano iliyopo katika utamaduni wangu ambayo inanifanya nikwepe kuingia na kukaa katika hali duni isiyovutia ya zizi la ng’ombe. Nitajaribu kujichunguza kwa uwazi na kuona jinsi ninavyoshiriki katika juhudi za ulimwengu huu za kuwapa makazi wasionayo, kuwavisha wasio na mavazi na kusaidia kwa hali na mali wote wanaoathirika na umaskini wa maisha ya mwanadamu.  Labda juma hili nitajaribu kufanya juhudi mahsusi za kujiona na kutenda kama nafsi yangu halisi ilivyo, kuwa muwazi zaidi.  Nitazingatia kuona jinsi siku inavyoweza kuwa iwapo nitajitahidi kuacha kuwaridhisha wenzangu kwa mambo na vitu ambavyo ni vya nje tu, wala havina mizizi moyoni mwangu—ila tu kuniwezesha kuwa au kusifiwa nao.

Kila siku ya juma hili, naweza kuchukua nyia tofauti ya kufanya marudio: kubaki katika sehemu fulani yenye zawadi zaidi, kuingia ndani ya neema fulani ili kupata muonjo wa zawadi ya Mungu kwa ukamilifu zaidi katika safari hii maalum ya kumwona Yesu kwa udhahiri zaidi, kumpenda kwa undani zaidi na kumfuasa kwa ukaribu zaidi, siku baada ya siku.

Kwa Ajili ya Safari: Usiharakishe Kuondoka

Mtakatifu Inyasi angependelea tutue na kukaa kwa muda katika ufukara na unyenyekevu wa zizi la ng’ombe alimozaliwa Yesu.  Mtoto Yesu anaanza kutoa maelezo yahusuyo utambulisho wake—maelezo yatuambiayo yeye ni nani.  Matukio ya humu zizini na hali inayotuzunguka ni maneno muhimu ya sentensi yake ndefu ya mapendo.

Tunapokaa humo tukiangalia yote, tunaweza kupitia dukuduku lolote tulilonalo kuhusu uwepo wetu humo ndani ya zizi. Uwepo wetu karibu naye haukwepeki iwapo kweli tunataka kuzijua njia zake.  Tuna haraka gani?  Tunamwangalia na kusikiliza.  Katika fikra zetu, tujiundie picha za rafiki zetu wakija kututembelea hapo zizini ambapo tumechagua kubaki kwa muda na mtoto.  Tutawaeleza yapi kuhusu yale tuliyoshuhudia kwa macho, masikio na uwepo wetu humo zizini?  Labda katika sala tunaweza kujisikia kutaka rafiki zetu wa zamani wakutane na hawa rafiki zetu wapya.  Tunahisi furaha na faraja moyoni tunaposogea karibu na pale Mariamu alipo kampakata mtoto?  Tunajihisi kuwa na heshima kiasi gani kwa Yusufu baada ya kushuhudia jinsi alivyoshughulikia tukio lote la uzazi wa mtoto—heshima hii inanifanya nihisi nini moyoni pale tunapoketi na Yusufu kuzungumza na wageni?

Kuna njia za kupata ukweli na njia tofoauti ya kukua katika kujua watu.  Yesu, Mariamu na Yusufu ni watu na Mt. Inyasi anatutaka tujitambue pia kuwa watu, na kama watu kuwa na uhusiano wa nafsi kwa nafsi na hawa tunaokutana nao hapa katika banda la wanyama, na wote tutakaokutana nao katika majuma yajayo.  Kuwa na uhusiano binafsi ni kujuana nao si kwa kutegemea kila kilichoandikwa au kusimuliwa na wengine, bali katika kuwaangalia, kuwasikiliza na kuwa karibu nao au kwa kifupi kujenga urafiki nao. Hata hivyo hili halitokei mara.  Katika njia ya kuwa marafiki, tunapitia hatua mbalimbali.  Yote huanza kwa kuangalia na kusikiliza na kupokea yoyote tunayopewa.  Tonaingia katika hatua ya kuwa watu wanaoelewana, halafu tunakuwa marafiki na kisha tunakuwa karibu zaidi kuliko marafiki, tunakuwa wenzi (waandani) au washirika.  Siku hizi tunajiweka wazi kuguswa moyoni na yale tunayoyaona na kuyasikia.

Ni muhimu kwetu kujikawiza kwenda mbele kwa kuwa ndani ya banda hili la wanyama, na kuanza kusogea taratibu kuelekea siyo tu lilipo hori la kulishia ng’ombe na alimo mtoto, ila pia ulipo ukweli wa tukio ambalo linaamua hatima ya ulimwengu mzima. Ni kipi cha maajabu ya Mungu wetu kinadhihirishwa kwetu katika hali hii ya kimaskini? Mungu mwenye upendo mkuu anaukumbatia ulimwengu kutokea hapa katika zizi dogo la ng’ombe na kuifikia hata sayari iliyo kubwa kuliko zote.  Mungu huyu anakuja katika zizi la ng’ombe la kila mmoja wetu kama kuna nafasi ambamo anaweza kumkaribisha.  Hajali hata kidogo uchafu na harufu ya zizi hilo.  Hii ni kusema, baada ya Betlehemu, hakuna jipya tena la kuonekana bali kueleweka.  Uamuzi wa Mungu siyo uamuzi wetu. Njia ya Mungu daima iko juu zaidi na kwa uamuzi wake, yaliyo muhimu ni yale yaliyo duni zaidi, na ni katika hali na sehemu duni ndipo ambapo wale tu walio wanyenyekevu wanaweza kuona na kuamini.

Hivyo tunaketi kwa muda kidogo katika rundo la nyasi za kulisha ng’ombe, na kuanza kukubali.  Kwanza tunaanza kumkubali yeye, na kumkubali kwetu kunaongezeka kila siku katika mazizi yetu.  Tunalikubali fumbo la ujio wake na ukweli kuwa haikuwa jinsi tulivyotarajia, kupanga wala kuamua—ni uamuzi wake.  Tunakubali kuwa tunapendwa na Mungu kwa namna ya ajabu.  Tunaanza kukubali kuwa njia za Mungu zinaanza kutuvutia.  Tunakubali kuwa tunahitaji kuongeza kidogo muda wa kuwa hapa ili kuangalia jinsi roho zetu zilivyoguswa na kunyanyuliwa na ujio wake katika namna tunayoshuhudia.

Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...

Yesu Mpendwa,

Nipo nyumbani. Nimetulia humu zizini nikiwa nawe na Mariamu na Yusufu.  Kuna baridi na harufu mbaya na nimesimama penye kinyesi cha ng’ombe, yawezekana pia nilikalia kinyesi cha ng’ombe bila kujitambua.  Hata hivyo nina furaha kubwa isiyo kifani.

Ni kama vile mara nyingi sipo tayari kukukaribisha kwangu.  Nahisi kuna wakati nimekuacha ukingoja nje kabla ya kukuruhusu uingie ndani; nimekuacha nje hadi nilifagie banda langu, nipate nyasi safi na kavu, nisafishe soli za viatu vyangu na kuweka tayari nguo za joto kwa ajili yetu sote.

Ningependa kuwa mwema zaidi. Hilo ndilo ninaloona katika giza la banda hili, giza la moyoni mwangu.  Sizungumzii mazingira ya hapa nilipo, ee Yesu, najizungumzia mimi na nafsi yangu. Nina wema wa kutosha kuwa mahali hapa nawe? Ni sasa tu ninapokuangalia wewe na wazazi wako ndiyo nahisi mapendo makubwa kwako—katika baridi na giza la humu kwenye zizi la ng’ombe.  Mikono yako midogo bado imekunya ngumi ya mtoto mchanga, na nipokusogezea kidole changu, unakikamata kwa nguvu: Bwana na Mwokozi wangu anaushika mkono wangu! Najawa na furaha moyoni hadi machozi ya furaha yananibubujika muda huu ninapojihisi kuwa rafiki wako wa ndani moyoni.

Mpendwa mtoto Yesu, kutoka mwanga hafifu wa humu kwenye zizi la ng’ombe nisaidie kuchungulia na kuona ndani ya giza la moyoni mwangu.  Nijalia kujihisi kwa undani zaidi kuwa hapa nipo nyumbani. Hapa mafanikio yangu makubwa kuliko yote ni kukupa kidole changu ukishikilie na kuking’ang’ania kitoto. Nisaidie nielewe kuwa hukuja kuwa nami katika hali iliyo na ukamilifu bandia, bali kuwa nami kama nilivyo sasa hivi: nyayo zikiwa zimezama katika mbolea ya ng’ombe, machozi yakibubujikia uso wangu wenye mavumbi, na kwa furaha natabasamia wazazi wako wanaosinzia karibu na ng’ombe mmoja na fahali wawili!

Yote haya hayaelekei kuendana na maisha yangu yaliyo katika mpangilio, hata hivyo nipo hapa katika hali isiyo kamilifu yenye kile kinachoonekana kuwa furaha kamilifu.  Moyo wangu umejawa shukrani nyingi kwa ajili yako, na kwa mapendo nainama kukutazama usoni.  Asante kwa kuwa wa maana kubwa sana maishani mwangu.  Asante kwa kunijia, na kutujia sote tukiwa katika mazizi yetu ya wanyama, tukiwa tumesimama gizani, tukiwa hatujui hasa nini cha kufanya.

 

MAFUNGO YA KIROHO KUPITIA MTANDAO