JUMA LA KUMI NA SABA

Namna Mbili za Kuwa na Shauku

Mwongozo: Tunataka Nini?

Tumeanza kutafakari maisha ya Yesu.  Tumeona jinsi, tangu hapo katika awali utoto wake, maisha yake yalijengeka katika kumtumainia Mungu, kujisalimisha katika mpango wa Mungu, na kukubali hali ya umaskini na kukataliwa. Tumekuwa tukisali ili kumjua, kumpenda na kuwa naye kwa undani zaidi.  Kabla hatujaendelea mbele kutafakari jinsi alivyotekeleza mwito wake mbele za watu, tunatenga majuma machache kujiweka katika hali ambayo mafungo haya yatakuwa na nguvu ya kuyagusa kwa ndani kabisa maisha yetu na kuyaekeza maamuzi tutakayokuwa tukifanya tutakapokuwa tunamkaribia zaidi Yesu.

Ni shauku ambayo hutuongoza katika kuchagua au kuamua.  Kuelewa maamuzi na chaguzi tunazofanya, na kujitayarisha kufanya maamuzi mapya, sharti tuzielewe shauku zetu na kuwa tayari kuzirekebisha ikibidi.

Juma lote hili, katika muda unaopata baada ya kumaliza shughuli fulani na kabla hujaanza nyingine, au uwapo katika kwenda sehemu ya shughuli inayofuata, au ukiwa katika mapumziko mafupi katika siku ambapo umebanwa sana na shughuli jaribu kuelewa jinsi ya kuwa na shauku au kiu inayotuweka pamoja na Yesu.  Huku tukijifunza kuikubali njia ya Yesu kwa uhuru, tutajaribu kuelewa nini hasa ni kinyume cha kuwa na shauku, njia ambayo tunaweza kusema inazinga tamaduni zetu mamboleo.

Ujumbe tunaopata kutoka katika mazingira ya jumuiya zetu siku hizi, na maadili ambayo yanatawala vyombo vya utangazaji ni wa kutushawishi kuwa tutakuwa na furaha zaidi tukiwa na mali zaidi. Mara nyingine ni shida kuuona wazi ujumbe huu kwa kuwa huweza kujificha sana katika yale yanayoonekana ya kawaida na ya kiasili; lakini msisitizo na ujumbe wake haubadiliki, ukitumia mantiki zenye kuvutia akili za wale wanaofikiri sana na pia vionjo vya wale wanaovutiwa na urembo wa nje.  Kwa mfano, matangazo mengi ya bidhaa yana ujumbe uliojificha kuwa ikiwa kiasi kidogo ni kizuri, basi kiasi kikubwa ni kizuri zaidi.  Inaonekana kuwa kawaida kufanya kazi zaidi ili kuwa na mapato zaidi kwa ajili ya kujipatia mali nyingi zaidi. Basi tunakuwa katika mzunguko wa kutafuta mapato na kuyatumia na hii hutuletea namna fulani ya mazoea mabaya au ulevi, na kwa wengine kuwa watumwa wa kazi na mapato, japokuwa kawaida tunachagua kuishi maisha yanayolingana na kipato chetu.  Tusifikiri kuwa ni mali tu ambayo tunaweza kujikusanyia.  Tunashuhudia tamaa ya kufaulu au kuwa na ustadi mwingi zaidi, kuwa na shahada nyingi za taaluma au kutenda yale ya kuvutia mahusiano na watu mashuhurivyote vikiwa viashirio vya mafanikio yetu.  Kisichofichika katika haya yote ni uhusiano usiokwepeka kati ya mali tunayomiliki na utambulisho wa nafsi zetu.  Tunakuwa katika kishawishi kikubwa sana cha kufikiri sisi ni zaidi kwa kuwa tunamiliki zaidi. Tunaanza kuwaweka watu wenzetu katika ya vipimo hivi vya mafanikio.  Japokuwa hakuna chochote kibaya kuhusu kuwa na mali au kuwa na mafanikio makubwa au kuwa mashuhuri mbele za watu, haya yote yanaweza kutuvutia kirahisi sana katika kuwa na majivuno, kiburi, na kujitenga na Mungu--mali kutuletea sifa, sifa kutuletea majivuno.  Ni vema kuuelewa vema mfumo huu wa shauku au tamaa, hasa iwapo unaendelea katika maisha yetu na ya jamii zetu.

Tayari tumeona kuwa mfumo wa Yesu ya kuwa na shauku ni tofauti kabisa.  Namna yake ya kufanya maamuzi inafanywa na mpangilio wa shauku ambao tayari umetuvutia na tunataka kuuelewa kwa undani zaidi juma hili.  Yesu anatuvutia katika shauku mama ya kumtegemea na kumwamini Mungu.  Tunapoyaweka maisha yetu katika mikono ya Mungu kama Yesu alivyofanya, tunashuhudia unyonge wa kujisalimisha huko. Pale tunapoona ukweli kuwa yote ni zawadi, hatuwezi tena kujipima kwa kiwango cha yale tuliyojikusanyia au kujilimbikizia.  Huu umaskini wa roho, na uhuru unaoendana nao mara nyingi vinaleta burudani ya pekee moyoni.  Yesu, hata hivyo, anatutaka tuelewe kuwa hili ni suala ambalo linapingana na tamaduni zetu—ni mapinduzi ya kitamaduni au ujenzi wa utamaduni unaopingana na tuliouzoea.  Kama mali hutuelekeza kwenye hutuletea sifa, basi umaskini wa aina yoyote sharti utakuwa ukituletea fedheha au aibu.  Sehemu kubwa ya jamii haithamini kumwamini Mungu pekee.  Baada ya shauku ya umaskini wa roho, kinachofuata ni umaskini halisi au umaskini wa mali, iwapo hili litakuwa jambo tunalozawadiwa.  Tutakavyotamani kutojipatia mali, ni kwa kadiri hiyo hiyo tutakosa dhamani mbele ya walimwengu.  Hivyo basi, shauku ya kumwamini Mungu pekee hutuongoza katika shauku kubwa ya kutokuthaminiwa, kudharauliwa na kuaibishwa ambavyo vinatuweka pamoja na Yesu.  Yote haya ni kwa kuwa hatimaye hii ni njia pekee ya kuelekea unyenyekevu na upole katika utumishi wowote pamoja na Yesu Kristu. Umaskini wa roho hutupeleka katika kudharauliwa, na kudharauliwa kunatujengea unyenyekevu.  Juma hili tunataka kuelewa njia hii ya kuwa na shauku.

Misaada inayofuata itatusaidia katika kuingia katika tafakari hii kwa ndani zaidi. Itatusaidia kuzianza tafakari hizi na kuzifanya ziwe sala.  Picha ya waathirika wa mabomu ya ardhini inaweza kutusaidia kutafakari kuhusu wale waliowekwe pembeni kabisa na jumuiya.

Zana za Kukusaidia Kuanza Juma Hili

Kutafakari namna mbili za kuwa na shauku juma hii ni rahisi sana kuliko inavyoweza kudhaniwa mara ya kwanza.  Haihusu kuchagua kujitenga na Mungu na kuungana na Yesu—tayari tumekwishafanya uchaguzi au uamuzi huo.  Tunachoomba juma hili ni neema za kutuwezesha kutambua namna za kuwa na shauku ambazo zipo hai zikituzunguka.  Mapokeo yetu ya Imani ya Kikristu tangu hapo awali yametuonyesha shauku hizi kama mapambano au vita kwa ajili ya roho zetu.  Juhudi yetu juma hili ni kuelewa mivutano na misukumo iliyo hai katika vita hivi vya kiroho.  Kuna mikakati miwili inayoshindana katika kuvutia mioyo yetu na katika kutuundia tabia ya kuwa na shauku au kutamani—hivyo hatimaye kuathiri maamuzi au uchaguzi wetu.  Neema za uhuru wa kiroho ambazo tunapewa zimejengeka katika busara tunayopata kutoka katika utambuzi wa misukumo hiyo ya ndani.

Tunachopaswa kufanya juma hii ni kuzitafakari namna hizo mbili.  Nikiwa nafanya lolote au nikiwa mahali popote, naweza kuwa nayarudia makundi haya mawili ya maneno: Mali-heshima-majivuno; Umaskini-fedheha-unyenyekevu.

Mwishowe natafuta njia za kuyaweka maneno haya katika hali yakinifu zaidi ili yaweze kuingiliana na maiya yangu ya kila siku:  Kuwa na vingi zaidi kunanifanya nijidhani ni mtu wa heshima zaidi, na hii inanifanya niwe na majivuno; kuwa na umaskini wa kiroho au umaskini wa mali kunanifanya nionekane nisiye na maana na nikikubali hili, najengewa unyenyekevu.

Nia yangu ya kujua nguvu hizi ndani ya maisha yangu inapewa nguvu na kukua kwa shauku yangu ya kumjua, kumpenda na kumtumikia Yesu.  Inatia matumaini na kusisimua sana kuona wazi jinsi Yesu, ambaye ananipenda sana na ananivutia niwe naye, ndiye anayenikomboa kwa kunipa utambuzi huo unaoniongezea shauku ya kutaka kuwa naye katika mfumo wake wa maisha.  Tukiwa waaminifu katika kufanya tafakari hii wiki nzima, tunaweza kuona wazi jinsi misukumo hii inavyofanya kazi katika maisha yetu ya kila siku. Tukiwa hapa tutaweza pia kuonjeshwa ladha ya shauku ya kufikia uhuru.

Tamaa yetu ya kuwa na Yesu inavyozidi kuongezeka, tunaweza kujaribu kujiundia akilini igizo lenye uhalisi katika maisha yetu: mtu aliyeacha utajiri ili amfuate Yesu—hili litaendana na kubezwa na marafiki wake, kutokueleweka na ndugu zake, kukanwa na kutelekezwa na wapendwa wake nk.—kisha nitajiuliza, “je, ni kweli kuwa nataka haya?”

Tunaweza kwanza kumgeukia Mariamu, mama mpendwa wa Yesu, ambaye tulitumia muda wetu kumtafakari katika majuma yaliyopita.  Tunaweza kumwomba amwombe mwanaye kwa niaba yetu, atupe neema hizi.  Hapa ni vema kuzitaja neema tunazohitaji.  Tunaweza kusema tunahitaji kuelewa njia hizi za kuwa na shauku na kupewa umaskini wa roho na hata umaskini wa mali kama hivyo vitatuwezesha kumtumikia Mungu zaidi na kusaidia kuokoa roho zetu.  Kama inasaidia, sala yetu kwa Mariamu inawenza kuhitimishwa kwa sala ya Salamu Maria.

Kisha tunaweza kumgeukia Yesu na kumwomba amwombe Mungu Baba, kwa niaba yetu, atupe neema hizo.  Iwapo tunaona ni vema sala yetu kwa Yesu imalizikie na sala ya ‘Sala ya Mt. Inyasi: Roho ya Kristu...’.

Mwisho, tunamgeukia Mungu na Baba yetu na kumwomba atupatie hizo neema. Sala inayofaa kuhitimisha mazungumzo yetu na Baba yaweza kuwa Sala ya Bwana (sala ya ‘Baba Yetu...’).

Tusisahau kwamba maendeleo yetu kiroho ni zawadi kutoka kwa Mungu, na vilevile zawadi moja hutufungulia njia kupokea zawadi zingine.  Tumeona jinsi neema tunazopokea zinatutayarisha kupokea neema mpya.  Tunachohitaji ni daima kuwa tayari kupokea na kuamini kuwa Yule aliyetufikisha hadi hapa katika safari hii ya kiroho ataendelea kuwa mhisani wetu mwaminifu hadi mwisho.

Kwa Ajili ya Safari: Sisi ni Nani?

Yesu anapobatizwa, anachuku nafasi yake au anaanza utume wake hadharani kama Mwana Mpendwa wa Mungu.  Tunatafakari tukio hili la kushangaza na kujiuliza iwapo tunataka kwenda naye.  Anaelekea kule ambapo atajaribiwa na shetani kwa kushawishiwa asitii Sauti ile aliyoisikia.  Anaendelea kuwa mtii akiitunza hadhi na hatima ya ubatizo wake. Katika maisha yake yote, atapata ‘miito’ mingine na kupewa ‘hadhi’ nyingi ambazo zitakuwa zikimvutia nje ya njia yake ya kuwa Mwokozi.

Katika hatua hii katika mafungo yetu, tunajaribu kuangalia jinsi tunavyoweza kulijibu swali linalowakabili watu wote, “Nawezaje kujua mimi ni nani?”  Utambulisho wetu ni dhaifu, na tunajiuliza mengi kuhusu nafsi zetu; na pia kutoka pembe mbalimbali tunapata mialiko mingi isiyoshabihiana juu ya jinsi ya kulijibu swali hili.  Kuna Yule Mwovu na jeshi la wafuasi wake, na kuna Yesu ambaye anatujia kwa amani na utulivu na kutupa mwaliko wake.

Tunasali juma hili ili kuelewa jinsi ambavyo mpango wa Yule Mwovu unatuvutia katika kujibu lile swali linalohusu utambulisho wetu.  Kwanza Roho Mwovu atajaribu kutuvutia kujibu hilo swali kwa kujilimbikizia mali ili kwamba tuweze kuona na kujiambia, “Ndiyo! Hakika mimi ninatambulika kwa hii miliki kubwa.”

Hivyo sala yetu inahusu jinsi tunavyoweza kuvutiwa na mali ambayo kwa upekee wake ni nzuri, ila sababu ya kuwa nayo inaweza kutia doa. Je tunaimiliki mali au inatumiliki sisi?  Yule kijana tajiri alijikuta mfungwa wa mali aliyokuwa nayo, kwa sababu mali yake ndiyo iliyomwambia yeye na watu wengine yeye ni nani.

Hatua inayofuata ni adui wa asili ya ubinadamu wetu anajaribu, baada ya kuona bado hakufaulu kutupa jibu kwa swali letu kwa kutumia mali tunayomiliki, sasa anakuja na pendekezo la kutupa nafasi muhimu katika jamii ambapo watu wengine watatuambia sisi ni nani.  Fahari na mamlaka vinavutia sana, na Yule Mwovu anamjaribu Yesu na sisi pia kujitambulisha na kujitambua kwa kutumia vyeo vyetu na hadhi mbele za watu.  Kusonga mbele namna hii ni kuendelea kukua katika kujitegemeza katika mambo yaliyo nje ya nafsi yetu ili kujijengea hadhi ya nafsi zetu.  Mtego wa tatu na wa hatari sana wa Kiongozi wa Uharibufu ni wa kutufanya tututumke kudai uhuru kutoka kwa Mungu.  Hii huanzia na kujiangalia sisi wenyewe kwa majivuno kuwa mipango na juhudi zetu ndizo zilizotufanya tuwe tulivyo na ndizo zinazotuendeleza katika maisha.  Hatumhitaji Mungu ila mali zaidi na watu wa kushuhudia uhodari wetu.

Tunageukia kambi ya Yesu, yule ambaye amesikia kutoka kwa Baba yake kuwa yeye ni nani hasa, na anatukaribisha tusikilize sauti hiyo hiyo ya uthibitisho katika ubatizo ikituambia kuwa sisi pia ni wapendwa wa Mungu.  Tumsikilize yule aliyetujaribu na kuona yote aliyokuwa anatupa; tunatumia muda kuona jinsi ilivyotuvutia kwa mialiko yake kutufanya kuamini sisi ni nani na kuwa hatuhitaji chochote kilicho nje yetu kutuhakikishia sisi ni nani—kumbe hali inayohitajika ni ya uhuru na uwazi wa kiroho, hali ambayo Yesu anaiita umaskini wa roho.  Tunajua mali ni nini, ipo kwa ajili gani na imetokea wapi.

Tunasikia kuhusu ‘uhuru kutoka...’ na ‘uhuru kwa ajili...’ vikifafanuliwa pale Yesu anapotualika tusijali pale ambapo tunapodhalilishwa au hata kufedheheshwa kwa kuwa majina yetu na utambulisho wetu vinapewa na Muumba wetu.  Uhuru kutoka katika mali na fahari za kidunia vinatusaidia kutembea katika njia huru ya Yesu, ambaye matendo yake na namna ya maisha tunatafakari juma hili.  Alijua yeye ni nani na anatuambia sisi pia katika siku hizi tujikubali kama wapendwa wa Mungu ili kwamba kumuiga yeye kuwe namna yetu ya kujitambulisha sisi ni nani.  Hatuishi kama nafsi zinazojitegemea tu, bali Kristu anaishi ndani yetu akifanya kazi kupitia nafsi zetu vile vile.

Juma hili tukutana uso kwa uso na namna ambazo tunavutiwa na hila na bidii za Mkuu wa Majaribu.  Tunakuta pia mioyo na akili zetu zikivutiwa kwenye njia na busara ya Yesu.

Katika Maneno Haya au Mengine Yanayofanana Nayo...

Mama Mariamu Mpendwa,

Nimetumia muda mwingi nikizungumza nawe tangu utoto wangu.  Sasa, ninapofanya mafungo haya, nahitaji kuwa karibu zaidi na mwanao, na najikuta nikitaka kufahamu wewe zaidi.  Katika majuma yaliyopita nilipokuwa nikisali, nimekuwa nikijiundia picha ya maisha yako na ulivyoyaishi pamoja na Yusufu na Yesu.  Naona jinsi ulivyomfundisha Yesu, na ninapokuona katika kazi nyingi kama mama, mzazi, mlezi, na mwanandoa, najikuta naweza kuhusiana nawe zaidi.

Nahitaji ndani moyoni mwangu kupokea neema ya ujasiri wa kuishi maisha yangu jinsi Yesu alivyoishi.  Tafadhali mwombe Yesu anipokee katika harakati za kumtumikia.  Naona namna nyingi ambazo nimejing’ang’aniza kwenye majivuno, kiburi na kumkana Mungu—hii ni njia yangu ya kujaribu kuwa Mungu. Tafadhali mwendee mwanao Yesu na kumsihi anisaidie kujikubali kama mdhaifu ili kwamba hii iwe chanzo cha neema katika maisha yangu.  Mahangaiko yangu ya kuwa mkamilifu hayatanifikisha karibu na Mungu, ila harakati zangu za kupokea mapungufu yangu yanaweza kunisaidia.

“Salam Maria, Umejaa neema...

 


Ee Yesu,

Nakugeukia kwa unyenyekevu.  Ninavutiwa sana na jinsi ulivyoishi duniani, ila inaonekana haiwezekani kwangu kuishi namna hiyo!  Nimebanwa katika kitendawili cha mahangaiko ya kidunia: kupata heshima na tunzo hapa na pale inaonekana vema ila haikidhi kiu yagu.  Najikuta natafuta kutukuka zaidi, kutambuliwa zaidi na watu wengi zaidi, sehemu nyingi zaidi.  Nimeyabadili maisha yangu ili yalingane na maoni ya walimwengu, na taratitu nimejikuta nazama katika upande tofauti wa maisha niliyotaka kuyaishi.

Hapo mwanzo nilijiuliza: namwumiza nani kama nikipata heshima kidogo kutoka kwa walimwengu?  Nilijiambia “tazama ni kushangiliwa kidogo na watu, watu kuniambia jinsi gani nilivyo hodari na mwerevu.”  Lakini sasa nimesoma mwongozo wa mafungo wa juma hili na najua kipi si sawa—jinsi gani ulimwengu ulikuwa mwerevu katika kunihadaa kubadili mtazamo wangu wa maisha.  Mara nilijikuta mimi mwenyewe ndiye heshima na tunzo za kila namna—kutukuzwa na walimwengu ndiko kunakoniambia mimi ni nani!  Je, kama hivi vikiondolewa kwangu au kufikia kikomo, mimi nitakuwa nani?  Nimepoteza nafsi yangu katika mbio hizi za kutafuta umaarufu na kutukuzwa, na sasa sina msimamo maishani.  Siyo kwamba kazi yangu ni mbaya au kwamba sifa zinadhuru; ila ni kwamba nimepoteza mtazamo wangu.  Mpendwa Yesu, mwombe Mungu Baba anisaidie kukataa yale ya hapa duniani ambayo yananizuia nisiwe na unyenyekevu na umaskini katika maisha kama uliokuwanao.

“Roho ya Kristu...

 


Mungu Mpendwa, Baba Yangu Muumba,

Umemtuma mwanao duniani kuwa mmoja wetu, kwa ajili yetu.  Nisaidie kuangalia jinsi alivyoishi na kuyafanya maisha yangu yafanane na yake.  Najua kwamba kwa sababu ya maringo na ubinafsi wangu napenda nifanye haya mimi mwenyewe, lakini sasa, ingalao kwa leo katika muda huu natambua kuwa siwezi.  Tafadhali, Ee Baba Yangu, nipe neema ya kumuiga Yesu katika yote, hata katika yale ambavyo yananitisha.  Siangalii tu katika sehemu za maisha zisizo za kawaida kama kuteswa na kusulibishwa, bali jinsi alivyoyapa kipaumbele mahitaji ya wengine, na si yake binafsi.  Baba mpendwa, nataka kuishi namna hiyo ila mara kwa mara najikuta niko mbali sana na njia hiyo ya maisha.

Kuwa nami katika harakati zangu za maisha.  Nipe nafasi niwe natafuta kibali chako tu cha jinsi ya kuyaishi maisha yangu.  Nijalie niweze kutambua njia za yule mwovu za kunihadaa na kunivuta kutoka katika kumfuasa mwanao, na kunifanya mtumwa wa malimwengu.

“Baba Yetu uliye mbinguni....

Maandiko Matakatifu:

Matayo            5:1-16

Wagalatia        5:16-26

Wafilipi           4:11-15

1 Timoteo        6:6-10, 17-19

1 Petro             5:1-11